31.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

MAKAMU WA RAIS AMSHUKIA RC SONGWE KWA KUMDANGANYA

 

Na IBRAHIM YASSIN, SONGWE


MAKAMU wa Rais, Samia Suluhu Hassan, ameiwata waongo na vilaza viongozi wa Mkoa wa Songwe baada ya kubaini kuwa walimdanganya na pia wameshindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo.

Akizungumza jana katika kikao cha majumuisho ya ziara yake ya siku tano mkoani humo, kilichowajumuisha watumishi  na viongozi wa Serikali, Samia alisema alidanganywa na Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Chiku Galawa.

Alisema baada ya kufika mkoani humo kwa ziara ya kikazi, Galawa alimwambia hawezi kutembelea baadhi ya maeneo ya mkoa huo kwa sababu barabara zake ni mbovu.

Samia alisema baadaye watendaji wa vyombo vyake walimpa taarifa kuwa kauli ya Gawala siyo ya kweli bali ililenga kumzuia asife katika baadhi ya maeneo ambayo hayana miradi ya maendeleo ya kuizundua.

Makamu huyo wa rais alisema amebaini Mkoa wa Songwe viongozi wake ni vilaza kwani licha ya kuwa na utajiri  wa madini ya dhahabu, hakuna mradi wa kuzindua.

Samia aliwataka viongozi wa mkoa huo kujitathimini utendaji wao kwa sababu kuna kila dalili kuwa wameshindwa kutimiza wajibu wao.

“Aliniambia mkuu wenu wa mkoa kuwa, Songwe ni mbali na barabara ni mbovu, lakini vyombo vyangu vimebaini kuwa alisema hivyo kwa sababu hapakuwa na mradi wa kuuzindua. Viongozi wa halmashauri wanaoongozwa na mkurugenzi ni vilaza,” alisema Samia.

Aidha, Samia alisema amebaini kuwapo kwa changamoto ya utawala bora mkoani humo na kuwataka viongozi wa mkoa kutoa mafunzo ya utawala bora katika ngazi ya halmashauri.

Aliuagiza uongozi wa mkoa huo kuanzisha program maalumu ya kupima afya za wananchi na kutoa elimu ya afya na uzazi wa mpango sambamba na kutunza mazingira kwa kupanda miti kwa wingi.

Katika hatua nyingine, Samia, aliwaasa wananchi wa Songwe  hususan wa Halmashauri ya Tunduma kuzaa kwa mpango.

Alisema akiwa Tunduma aliona watoto wengi wa shule waliofika kumlaki wakiwa pembezoni mwa barabara wakiwa na majani jambo linaloashiria kuwa wananchi wa wilaya hiyo hawazingatii uzazi wa mpango.

Makamu wa Rais, Samia jana alimaliza ziara yake ya kikazi ya siku tano mkoani Songwe kwa kutembelea vituo vya afya, mradi wa maji, shamba la miti pamoja na kuzungumza na watumishi wa Serikali.

Baada ya kikao hicho, alielekea mkoani Mbeya alipokelewa na umati mkubwa wa wananchi wa Wilaya ya Mbalizi ambao aliwapa pole kwa kuandamwa na ajali za barabarani.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles