28.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Makamu wa Rais ahimiza utunzaji mazingira

bi-samia-suluhuPatricia Kimelemeta

MAKAMU wa Rais, Samia Suluhu amewataka wananchi kutunza mazingira ili kuepusha athari za mabadiliko ya tabianchi ambazo zinaweza kuhatarisha maisha ya binadamu na mifugo.

Akizungumza jana kwenye mkutano wa Kigoda cha Mwalimu Julius Nyerere Dar es Salaam jana, Samia alisema bila ya kufanya hivyo, nchi inaweza kupata matatizo mbalimbali ikiwamo ukame na baa la njaa.

Alisema, kitendo cha kukata miti ovyo na kufanya uharibifu katika shughuli za binadamu kumechangia kuongezeka kwa nyuzi joto 0.84, jambo ambalo ni hatari kwa maisha ya kila siku.

“Wananchi wanapaswa kuacha mzaha katika suala hili, kwa sababu tuendako kunaweza kuhatarisha maisha yetu, hivyo basi kila mmoja anapaswa kuwa balozi wa kuhamasisha shughuli za utunzaji wa mazingira na kupanda miti ili kuzuia mabadiliko ya tabianchi na ukame,”alisema Samia.

Alisema jitihada za makusudi zinahitajika ili kuinusuru nchi isiweze kuingia katika matatizo hayo, hali inayoweza kusababisha kuongezeka kwa jangwa, ukame na njaa.

“Mkoa wa Kagera ni miongoni mwa mikoa ya mfano ambayo haijawahi kuathiriwa na njaa, lakini mwaka huu tumeona hali ilivyo mbaya… tatizo hilo lote linatokana na uharibifu wa mazingira,”alisema.

Alisema hadi sasa, Serikali imefanya maboresho ya sera ya mazingira ili iweze kutoa fursa kwa wananchi kuibua mambo ya kupambana na hali hiyo, ikiwamo kupanda miti, kuhifadhi vyanzo vya maji na mengineyo.

Akimnukuu Papa Francis wa 16 aliyekua akizungumza kuhusu mazingira, aliwataka wananchi duniani kote kuwa rafiki na mazingira kwa sababu hayasamehi, tofauti na Mungu ambaye ukimwomba msamaha anasamehe.

Alisema, vitendo vya uharibifu wa mazingira vinapaswa kutokuwa rafiki na binadamu kwa sababu vinachangia kuongezeka kwa mabadiliko ya tabianchi.

Kwa upande wake, NaibuWaziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Mhandisi Stella Manyanya, alisema Serikali inapaswa kuandaa mitalaa ambayo itatoa elimu ya utunzaji wa mazingira kuanzia ngazi ya awali hadi vyuo vikuu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles