25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Majaliwa: Tanzania kuna uhuru wa habari

Mwandishi wetu – Dar es Salaam


WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa, amesema Tanzania hakuna ubanaji wa uhuru wa vyombo vya habari wala taasisi zisizo za kiserikali.

Alisema hali hiyo inadhihirishwa na kuwapo  vituo 152 vya radio   ambavyo kati yake vitatu tu ndivyo vinavyomilikiwa na Serikali.

Majaliwa alisema hayo katika maadhimisho ya siku ya Umoja wa Mataifa yaliyofanyika kwenye viwanja vya Karimjee   Dar es Salaam.

“Serikali ya Tanzania inaongozwa na katiba na sheria za nchi ambazo zinatoa uhuru wa kujieleza na kupata habari,” alisema.

Alisema mwananchi yeyote atakayeenda kinyume na sheria, Serikali itamuwajibisha kwa mujibu wa sheria.

Alisema Serikali imeridhia mkataba wa kimataifa wa haki za raia na ule wa haki za uchumi, jamii na utamaduni.

Majaliwa alisema sambamba na kusimamia haki hizo, Serikali imeendelea kutekeleza wajibu wake katika kuiwezesha jamii kuishi salama kwa amani na utulivu kwa kuzingatia sheria za nchi.

Alisema kukuza, kuimarisha na kulinda haki za binadamu ni wajibu wa Serikali na kwa kuzingatia umuhimu huo mwaka 1984 iliingiza sheria ya haki za binadamu katika katiba.

Alisema pia kuwa urejeshaji wakimbizi wa Burundi kwao lilikuwa ni suala la hiari na limetekelezwa baada ya hali ya amani kurejea.

Alisema hakuna sababu ya kuendelea kuwahifadhi wakimbizi ambao kwa hiari yao wameamua kurejea nchini kwao.

“Tangu Septemba mwaka jana, Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Burundi na UNHCR imekuwa ikiwarejesha wakimbizi hao kwao.”

Alisema wakimbizi 52,283  wa Burundi walirejea nchini kwao kati 81,281 waliokwisha kujiandikisha.

Alitoa wito kwa jumuiya ya kimataifa na washirika wengine wa maendeleo kuendelea kushirikiana na Tanzania kwa mujibu wa mkataba wa UN wa mwaka 1967 wa kuwahudumia wakimbizi  kufanikisha kuwarejesha makwao kwa hiari na kwa kuzingatia misingi ya haki za binadamu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles