23.3 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

MAJALIWA AMWAGIZA SENDEKA AKUNJUE MAKUCHA

Na Mwandishi Wetu- Njombe

WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa, amemwagiza Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Christopher ole Sendeka, kuwachukulia hatua watumishi wa Ludewa waliohusika na upotevu wa fedha za maendeleo.

Kauli hiyo aliitoa juzi jioni alipozungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Uwanja wa Halmashauri.

Alisema zaidi ya Sh milioni 700 zilipelekwa katika halmashauri kwa miradi mbalimbali ya maendeleo zikiwamo Sh milioni 300 za ujenzi wa ofisi ya halmashauri hiyo.

“Mkuu wa Mkoa watu wote waliohusika na upotevu huu watafutwe popote walipo na kuchukuliwa hatua na kisha nipewe taarifa ya hatua ulizochukua. Hatuwezi kuwavumilia watu hao ambao wanachora ramani kwa shilingi milioni 200 na shilingi milioni 100 nyingine hazijulikani zilipo,” alisema.

Pia alimwagiza Sendeka kufuatilia kiasi kingine cha Sh milioni 400 zilizopelekwa wilayani hapo kwa ajili ya maendeleo ambazo nazo hazijulikani zilipo.

“Tafuta waliohusika popote walipo hata kama ni nje ya Njombe waje kutueleza ziliko fedha zetu,” alisema.

Licha ya kutoa agizo hilo kwa Sendeka, pia ameuagiza uongozi wa Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (Takukuru), kuhakikisha inashirikiana kufanya uchunguzi ili kubaini watu waliohusika na upotevu huo.

Katika hatua nyingine, alisema Serikali haitawavumilia watumishi wote wanaojihusisha na vitendo vya ubadhirifu wa fedha za umma.

Aliwataka watumishi wa umma kuacha tabia ya kudokoa fedha za maendeleo zinazopelekwa katika halmashauri zao kwa sababu Serikali iko macho na itawashughulikia wote watakaobainika kujihusisha na vitendo hivyo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles