25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

MAHREZ AMEANZA KUUPANDA MLIMA ALIOUHOFIA

ADAM MKWEPU NA MITANDAO

WAKATI vigogo wa soka barani Ulaya vikisubiri kufunguliwa kwa dirisha la usajili mwezi ujao, winga wa Leicester City, Riyad Maharez, tayari ametangaza  kutafuta timu nyingine ya kucheza msimu ujao na kutaka kuachana  na aliyokuwa akiichezea msimu uliopita.

Kila mmoja anamkumbuka fundi huyu wa mpira wa kukimbizana na upepo, wakati huo timu yake ilipotwaa ubingwa wa Ligi Kuu England mwaka jana, msimu wa 2015/16 na mwaka huu kuibuka na tuzo ya mwanasoka bora.

Hakuna tena kelele juu yake, pengine ukurasa kuhusu mustakabali wake kwa klabu zilizokuwa zikimhitaji ungekuwa umemalizwa kwa makubaliano ya fedha ndefu, si hii ya madafu ambayo anaweza kuipata kwa sasa kutoka kwa Arsenal au klabu nyingine zinazotaka kumsajili.

Wakati huo, nyota ya Mahrez ilikuwa iking’aa hadi kusababisha kuhusishwa kuhamia kwenye klabu ya Arsenal, Chelsea na Monaco.

Kuna gazeti moja la nchini Hispania liliwahi kuandika kuwa usajili wa Mahrez ulikuwa ni miongoni mwa sajili kubwa kutarajiwa kufanywa na klabu hiyo katika misimu miwili iliyopita.

Yapo mambo mazuri ambayo kwa sasa yanaonekana kusahaulika kuhusu Mahrez, kwamba aliwahi kuchukua tuzo ya mchezaji bora England, alikuwa miongoni mwa wachezaji waliochangia kuendelea kusalia katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu uliomalizika.

Mahrez ana uwezo wa kukaa na mpira, kutoa pasi, kuzungusha anavyotaka na kufunga bao muda anaotaka kwa sababu ya kipaji chake.

Namna anavyocheza na mpira ni hatari nyingine mbele ya timu pinzani, hata hivyo, kwa sasa anaonekana kama kukwazwa na mwenendo wake au timu aliyokuwa nayo kushindwa kufanya vizuri msimu uliopita.

Mahrez ni miongoni mwa stori nzuri inayosisimua miongoni mwa wapenda burudani ya mpira, ikisimulia kuanzia Ligi Daraja la kwanza hadi Ubingwa wa Ligi Kuu England na mchezaji bora wa mwaka.

Na ghafla kuonekana si lolote nje ya Ligi Kuu England. Mashabiki wa nyota wa Barcelona, Lionel Messi na wachezaji wa  Atlético Madrid, waliwahi kuimba wimbo wa kumsifu Mahrez, wakimwita “a craque”, wakimfananisha na kitu cha kipekee, hiyo ni kabla ya robo fainali ya michuano ya Mabingwa Ulaya mwaka jana.

Ndani ya England inaonekana kwamba huenda Mahrez anakwamishwa na baadhi ya vitu vinavyomzunguka katika maisha yake binafsi nje ya uwanja.

Hakuna shaka kwamba Mahrez ni aina nyingine ya wachezaji kulingana na  uchezaji wake inayovutia wengi katika soka la ushindani na burudani.

Wapo wanaosema Mahrez ana aina moja tu ya uchezaji, akitumia mguu wa kushoto kufanikisha anachotaka na kama ukiweza kuinasa mbinu yake hiyo ana kuwa kama kamwagiwa maji ya baridi.

Lakini mbinu zote hizo zimejikita katika uwezo wake wa kukimbia na kusimama  ghafla na kwa haraka huangalia sehemu sahihi ya kuupiga mpira, jambo hilo amekuwa akilifanya kwa ustadi mkubwa kuliko mchezaji yeyote ndani ya uwanja.

Nguvu anayotumia inawiana na ubunifu unaomfanya kuwa wa kipekee anapotaka kulifanya jambo lake dhidi ya timu pinzani.

 Jina ‘mchezaji’ linaweza kutajwa vibaya katika soka, wachezaji wa kulipwa hawachezi tu soka, wanafanya zaida ya inavyotakiwa kufanya ili kuucheza mpira ndani ya uwanja.

Ukianzia kwa nyota wa Real Madrid,  Sergio Ramos anavyofanya kuhusu  mpira ufanye vile anavyotaka.

Ni ngumu kufikiri kwamba soka la England linamalizana na mchezaji kwa aina ilivyofanya kwa Maharez.

Mkongwe mmoja katika soka, Chris Waddle, anasema kwamba, Mahrez anamkumbusha nyota wa soka wa Kibrazil aliyetambulika kama ‘Great Djalminha’, aliyetokea miaka ya 90,  wakati akicheza soka lake nchini Hispania ‘La Liga’.

Nyota huyo alikuwa anaweza kuufanya mpira vile anavyotaka na kukuacha ukicheka kutokana na kile kinachotokea ndani ya uwanja.

Huenda Mahrez akasalia kwenye Ligi Kuu England. Labda akachukuliwa na kocha wa timu ya Arsenal, Arsène Wenger, baada ya kupewa pauni milioni 150 za kusajili.

Linaweza kuwa jambo zuri au uamuzi mbaya kama Wenger asipomsajili nyota huyo baada ya kumkosa nyota wake, Santi Cazorla.

Zaidi ya hapo, Mahrez anawakilisha jambo jingine zaidi ya uwezo unaoonekana na wengine ambapo ni sanaa ya mchezo wa soka.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles