KULWA MZEE-DAR EA SALAAM
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, imemuachia huru Mkazi wa Magomeni Makuti, Kihemba Mchungu, aliyekuwa anatuhumiwa kufanya biashara ya dawa za kulevya, baada ya Jamhuri kushindwa kuthibitisha mashitaka na kushindwa kuwafikisha mashahidi muhimu mahakamani.
Hukumu hiyo ilitolewa jana na Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Maira Kasonde.
Hakimu Kasonde alisema upande wa Jamhuri uliwasilisha mashahidi sita mahakamani ambao katika ushahidi wao walieleza kwamba walienda kufanya upekuzi kwa mshtakiwa Februari 3 mwaka 2018 na walikuta vitu mbalimbali ukiwamo mfuko wa nailoni mweusi uliosadikiwa kuwa na heroine.
Alidai katika upekuzi huo walikuwa na mashuhuda Hussein Choki na Sharifa Mrisho ambao waliwaamsha usiku wa manane kwa ajili ya upekuzi.
“Mshtakiwa katika kujitetea alidai upekuzi ulifanyika bila yeye kuwapo, ushahidi wake uliungwa mkono na Sharifa Mrisho ambaye anadai alipofika nyumbani kwa mshtakiwa alimkuta yuko nje kafungwa pingu na askari wengine wako ndani ya nyumba yake.
“Sharifa anakana kuona mfuko wa nailoni unaosadikiwa kuwa na dawa za kulevya nyumbani kwa mshtakiwa na kwamba polisi walitaka atoe ushahidi, alikataa baada ya kuona walitaka aseme mfuko wa nailoni ulikutwa kwa mshtakiwa wakati wa upekuzi.
” Alipokataa alikamatwa na kukaa mahabusu siku nne, mwenyewe anadai hilo lilikuwa jaribio la kutaka aseme mfuko ulikutwa kwa mshtakiwa lakini alikataa,”alisema Hakimu.
Hakimu Kasonde anlisema upande wa utetezi umewekea shaka ushahidi wa Jamhuri na kwamba ulipaswa kuungwa mkono sababu shaka iko katika upatikanaji wa kielelezo hicho cha dawa za kulevya.
“Katika kesi hii Mahakama haikuelewa kwa nini Jamhuri haikuwaita mashuhuda wa upekuzi Sharifa na Hussein kama mashahidi kwa sababu hao walikuwa mashahidi muhimu.
“Mashahidi hao hawakuitwa na hakuna siku ambayo Jamhuri waliomba hati ya kuwaita mashahidi hao.
“Hii inaweza kufikiriwa kwamba walihofia kuwaita kwa vile wangekuja wangesema tofauti,”alisema Hakimu Kasonde.
Alisema kutokana na shaka hiyo ya upatikanaji wa nailoni inayosadikiwa kuwa na dawa za kulevya na upekuzi kufanyika kinyume na utaratibu, Mahakama inamuachia huru mshtakiwa, haki ya kukata rufaa iko wazi,”alisema.
Mshtakiwa aliachiwa huru kwa mujibu wa kifungu cha sheria namba 235 cha Mwenendo wa Makosa ya Jinai sura ya 20.