24.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 16, 2024

Contact us: [email protected]

Magufuli asema yeye ndiye mshindi

mtz1FINALNA BAKARI KIMWANGA, CHALINZE

MGOMBEA urais wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. John Magufuli, amesema anajua yeye ndiye rais wa awamu ya tano na Watanzania wameshamhakikishia watamchagua keshokutwa wakati wa kupiga kura.

Kwa mujibu wa Dk. Magufuli, anajua Watanzania wamechoshwa na ahadi za uongo, na kwamba sasa wanahitaji ahadi za vitendo.
Dk. Magufuli aliyasema hayo jana katika mkutano wa kampeni uliofanyika Chalinze, Mkoa wa Pwani.
“Watu wamechoshwa na ahadi za uongo na wanahitaji matumaini mapya, na mimi nasema nichagueni, sitawaangusha na sadaka yangu kwenu ni kufanya kazi kwani kwangu ni kazi tu.

“Nataka nifanye kazi, sitawaangusha kwani nimefanya kazi kwa miaka 20 kwa niaba yenu Watanzania.
Nimewahi kulala kwenye madaraja na kila mmoja anajua uchapakazi wangu.

“Nitafanya kazi kwa uadilifu kwa sababu nina hofu ya Mungu na wakati wote nitamuomba ili nisiwaangushe,”
alisema Dk. Magufuli.

Katika hatua nyingine, Dk Magufuli alisema anashangazwa na maneno yaliyotolewa na mgombea urais wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa, kuhusu ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo.

Amesema kwamba kauli ya Lowassa ya kuhoji fedha za ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo kama zilitolewa kwa mkataba haiwezi kukubalika kwa kuwa anapanga kuufuta mkataba huo pindi atakapoingia madarakani.

Kwa mujibu wa Dk. Magufuli, kauli ya Lowassa inalenga kuleta chuki kati ya wananchi wa Bagamoyo na Tanga, na kwamba inawezekanaaliitoa kwa kuwa anajua Rais Jakaya Kikwete ni mzaliwa wa Bagamoyo.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Magufuli hakutaja jina la Lowassa, lakini maelezo yake yalimlenga mgombea urais huyo wa Chadema kwa kuwa alipokuwa jijini Tanga juzi, alisema ataangalia mkataba wa ujenzi wa bandari hiyo baada ya kuingia madarakani ili fedha zilizotengwa, zihamishiwe katika ujenzi wa Bandari ya Tanga.

“Mimi sitoki Bagamoyo ila nasema hapa iwe usiku au mchana, Bandari ya Bagamoyo itajengwa kwani inajengwa na watu binafsi kupitia mpango wa pamoja kati ya Serikali na Sekta Binafsi (PPP).

“Tutajenga Bandari Mtwara, Tanga na Mwanza na fedha zipo. Hata fedha za Bandari ya Tanga nazo zipo na tutaijenga pia. Msikubali kuchonganishwa na watu kwa maneno ya ubaguzi, kwani wanayasema haya kwa sababu
Rais Jakaya Kikwete anatoka Bagamoyo,” alisema Dk. Magufuli.

Akizungumzia miundombinu, Dk. Magufuli, alisema Serikali itajenga barabara kubwa ya kisasa ya njia sita kutoka Chalinze hadi jijini Dar es Salaam.

Alisema ujenzi wa barabara hiyo utakuwa na barabara za juu saba zitakazojengwa kwenye maeneo ya Chalinze, Mlandizi hadi jijini Dar es Salaam.

“Tutajenga ‘Fly over’ saba kuanzia hapa Chalinze hadi Dar es Salaam na tayari fedha za mradi huu zimeshatengwa kiasi cha shilingi trilioni 2.3.

“Kutokana na hali hii, sasa maendeleo yanakuja kwa kasi na ninawaomba sana msiuze ardhi yenu kwani Chalinze na Kibaha mpya yenye maendeleo inakuja kwa mujibu wa sheria ya ardhi ya mwaka 1999 pamoja na ile ya matumizi
bora ya ardhi.

“Wasije wajanja wakawarubuni kwa kuwakatia maeneo yenu kwa shilingi 50,000 kisha wanakuwa na maeneo makubwa na watakapokuja wawekezaji, wanayauza kwa fedha nyingi,” alisema Dk. Magufuli.

Kuhusu sekta ya elimu, alisema kazi kubwa iliyofanywa na Rais Kikwete ni kujenga madarasa ya kutosha, na kwamba atakapoingia madarakani, ataboresha elimu na masilahi ya walimu.

“Kazi kubwa imefanywa na awamu ya nne na mimi ikiwa mtanichagua Jumapili kwa kura nyingi
na kuwa rais wenu, nitaboresha elimu baada ya kujenga shule za kata,” alisema.

Dk. Magufuli yupo katika kampeni za lala salama ambapo jana alifanya mikutano kwenye majimbo ya Kibamba, Kibaha Mjini na Vijijini, Chalinze na Kawe.

KIKWETE PEMBA

Kutoka Pemba, Nora Damian anaripoti kuwa Rais Jakaya Kikwete amesema hawaiingilii Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) bali wanachofanya ni kuiwezesha kupata fedha ili itimize majukumu yake. Kauli hiyo aliitoa Kisiwani Pemba
jana wakati wa kufunga kampeni za CCM zilizofanyika katika Uwanja wa Gombani ya Kale uliopo Mkoa
wa Kusini Pemba.

“Matayarisho ya uchaguzi ni kazi ya NEC hatuwaingilii, jukumu letu ni kuwawezesha kupata fedha na tumefanya hivyo ndiyo maana mmeona vifaa vimesambazwa,” alisema Kikwete.

Alisema uchaguzi utafanyika kwa amani na utulivu na kuonya kuwa atakayejaribu kufanya vurugu atachukuliwa hatua.
Naye mgombea urais wa Zanzibar kupitia CCM, Dk. Ali Mohamed Shein, alisema endapo atachaguliwa tena yale yote aliyoyaahidi yatatekelezwa

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles