24.1 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Magufuli aitikisa Muhimbili

John+Magufuli+PHOTO*Uongozi wahaha siku za mapumziko

* Sefue leo kufanya ukaguzi, kufuatilia maagizo

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

UAMUZI wa Rais Dk. John Magufuli kumng’oa aliyekuwa Kaimu Mkurugenzi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dk. Hussein Kidanto, umesababisha wafanyakazi wa hospitali hiyo   na viongozi wao kufanya kazi hadi  siku za mapumziko.

Hatua hiyo imekuja wiki chache baada ya Dk. Magufuli, kufanya ziara ya kushtukiza hospitalini hapo, Novemba 9 ikiwa ni ziara yake ya pili baada ya ile aliyoifanya Wizara ya Fedha.

Katika ziara hiyo, Dk. Magufuli alichukua hatua kadhaa ikiwamo ya kumhamishia Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii aliyekuwa Kaimu Mkurugenzi wa Hospitali hiyo, Dk. Hussein Kidanto.

Dk. Kidanto alikaimu nafasi ya Ukurugenzi mapema mwaka huu baada ya aliyekuwa Mkurugenzi, Dk. Marina Njelekela, kustaafu kwa mujibu wa sheria.

 

Vilevile alimteua aliyekuwa Mkurugenzi wa Taasisi ya Mifupa (MOI), Profesa Lawrence Mseru kuwa kaimu mkurugenzi kuanzia Novemba 10.

Taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu Novemba 9  mwaka huu, ilieleza kuwa Rais Magufuli alikasirishwa na hali ya kutokujali wala kushughulikia vifaa vya kufanyia kazi.

Ilisema katika ziara hiyo, Rais alikuta mashine muhimu za uchunguzi wa magonjwa kama vile MRI na CT-SCAN zikiwa hazifanyi kazi kwa   miezi kadhaa wakati  mashine kama hizo   zinafanya kazi katika hospitali binafsi na wagonjwa wanaelekezwa kwenda kutafuta huduma huko.

Kutokana na hali hiyo, Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue alitoa maagizo ya Rais Magufuli ya kuvunja Bodi ya Hospitali ya Taifa ya Muhimbili ambayo ilikwisha kumaliza muda wake.

Taarifa kutoka ndani ya hospitali hiyo jana zilisema  tangu Rais Magufuli afanye ziara hospitalini hapo, viongozi wa ngazi za juu  wamekuwa wakifanya kazi pamoja na vikao vya mipango ya maendeleo hadi   siku za mapumziko katika wiki.

“Ninapozungumza nawe hivi sasa wakubwa wote wapo kazini na hili naliona linafanyika wiki ya pili sasa.

“Jumamosi na Jumapili  viongozi wote na Kaimu Mkurugenzi (Profesa Mseru), wanakuwapo kazini wakiendelea na majukumu yao ya kawaida.

“Nafikiri hili linatokana na mkakati wa Rais Magufuli wa  kuhakikisha Muhimbili inakuwa  kimbilio la kila Mtanzania na si vinginevyo.

“Jana (juzi) vililetwa vitanda hapa kwa agizo la Rais Magufuli na vyote leo (jana), tumekuwa katika kazi ya kuvifunga na kuwalaza wagonjwa waliokuwa wamelala chini,” alisema mtoa habari wetu.

MTANZANIA ilimpomtafuta Meneja Uhusiano wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Aminiel Eligaesha, alisema suala la viongozi wa juu wa Muhimbili kufanya kazi  hata katika siku za mapumziko ni la kawaida kwao.

“Hili la vikao na kuendelea na majukumu kwa viongozi wetu wa hospitali ni suala la kawaida katika kutekeleza majukumu … ila hili la vitanda siwezi kuzungumzia kwa sababu vimetolewa kwa upande wa MOI na si kwetu Muhimbili,” alisema Eligaesha.

 

Sefue kutua leo

Ratiba iliyotolewa jana na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais Ikulu, ilieleza kuwa katika kuhakikisha maagizo ya Rais Magufuli yanatekelezwa, leo Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue atafanya ziara  kukagua na kuhakikisha kama vitanda vyote vilivyopelekwa hospitalini hapo vimefungwa na wagonjwa wanavitumia.

Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Gerson Msingwa alisema Balozi Sefue  atafanya ziara  Muhimbili leo saa 4.00 asubuhi.

“Mnaarifiwa kuwa Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue atafanya ziara katika Hospitali ya Taifa Muhimbili kesho (leo), Jumatatu  kuanzia saa nne asubuhi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles