Na HERIETH FAUSTINE-DAR ES SALAAM
JESHI la Polisi, Kikosi cha Usalama Barabarani, limetoa taa 665 za mwanga mkali (Sports light) ambazo zilikuwa zikitumiwa na vyombo vya usafiri na kusababisha ajali.
Taa hizo zilitolewa katika malori, magari madogo, pikipiki, baada ya kushindwa kutoa wenyewe kama walivyoamriwa awali.
Hatua ya kuondoa taa hizo ilitokana na kuwapo kwa malalamiko kutoka kwa madereva barabarani ambao walidai kuwa taa hizo zimekuwa zikiwasababishia upofu wa muda na kushindwa kuona mbele na kusababisha ajali kutokea.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Kamanda wa Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani, Mohammed Mpinga, alisema taa hizo zilikuwa zikitumika vibaya hasa nyakati za usiku na kuwa chanzo cha ajali nyingi za barabarani.
Alisema matumizi ya taa za mwanga mkali yalikuwa yakiongezeka, ambapo kwa mwaka 2015 yalisababisha ajali 104 na kwa mwaka jana ziliongezeka na kufikia 123.
“Kutokana na kuonekana kuwa ni moja wapo ya sababu za ajali barabarani, ni kinyume cha sheria kufunga taa hizi katika gari na ni hatari zaidi hasa zinapotumika bila kujali watumiaji wengine wa barabara.
“Yawezekana gari likafungwa taa hizi kutoka kiwandani kwa makusudi maalumu, lakini dereva huzitumia kinyume na makusudio yake na kuwa hatari kwa watumiaji wengine wa barabara,” alisema Kamanda Mpinga.
Alisema katika utafiti uliofanywa, ilibanika kuwa Mkoa wa Singida ndio unaoongoza kwa kuwa na matumizi ya taa hizo, baada ya kukamata magari 170 yaliyokuwa yamefungwa taa za mwanga mkali.
Kwa upande wa magari madogo, Kamanda Mpinga aliwataka pindi wawapo mjini kuvalisha kava taa hizo ili zisiweze kusababisha ajali.
“Nawaomba wenye magari madogo wakati wakiwa mjini wazifunike taa hizo na makava na wakikaidi amri hiyo tutawakamata na kuzitoa wenyewe,” alisema.
Kamanda Mpinga alisema watashirikiana na Shirika la Viwango Tanzania (TBS), ili kuweza kutunga kanuni ambazo zitawabana wanaotumia vibaya taa barabarani ili kuweza kupunguza ajali zinazosababishwa na matumizi mabaya ya taa hizo.