Na Sheila Katikula, Mwanza
Mafundi umeme wametakiwa kujisajili na kupewa leseni na Mamlaka ya Udhibiti ya Huduma za Nishati na Maji (EWURA) ili kuzuia ajali za moto zinazosababisha vifo na uhalibifu wa mali sanjari na kuepuka vishoka.
Akizungumza na www.mtanzania.co.tz , Meneja wa Mamlaka ya Udhibiti ya Huduma za Nishati na Maji ( EWURA) Kanda ya Ziwa, George Mhina, alisema lengo la utoaji wa leseni za kuunganishia mifumo ya umeme kwa mafundi hao itasaidia kila mtu kufikiwa na nishati hiyo kwa uhakikika na usalama.
Alisema hadi sasa zaidi ya mafundi 3,500 wamesajiliwa kwa nchi nzima na kupewa leseni ili waweze kufanya kazi kwa uhakika kwani kufanya kazi bila leseni ni kosa na adhabu zitachukuliwa ikiwemo kifungo cha miaka mitano au faini isiyozidi sh milioni 10 au adhabu zote mbili kwa pamoja.
“Maombi ya leseni hufanywa mtandaoni kupitia mfumo wa Lois katika tovuti ya mamlaka hiyo zinatolewa kulingana na sifa za mwombaji ambapo daraja A ni fundi mwenye uwezo wa kufanya kazi zote za ufungaji na usambazaji umeme, daraja B ufungaji umeme msongo wa kati hadi volti 33,000.
“Kwa daraja C fundi anakuwa na leseni ya ufungaji umeme usiozidi volti 400, na mwombaji anapaswa kuwa na nakala ya picha ya rangi ya bluu (pasipoti), kuambatanisha Wasifu (CV)na nakala ya vyeti vya elimu ya ufungaji umeme hati ya kusafiria, kitambulisho cha taifa,” alisema.
Hata hivyo Mbina amewataka wananchi kuhakikisha wanaweka utaratibu wa kukagua nyaya za umeme kwenye nyumba zao ili kuweza kubaini kama zimechubuka na kuzibadilisha ili kuepuka majanga ya moto.
“Hivi karibuni tumeshuhudia shule zikiungua na kusababisha vifo na mali kuteketea, sheria inasema kila baada ya mwaka mmoja unapaswa kuangalia nyaya kama zipo vizuri kwenye nyumba na kumbi za starehe na kwenye shule kila baada ya miaka mitano.
“Kwa viwandani kila baada ya miaka mitatu inashauriwa zoezi hilo ili kuepuka na changamoto hiyo ni vema kuweka utaratibu wa kukagua nyaya kama sheria zinavyosema,” alisema Mhina.
Mhina alisema kwa mjibu wa kanuni zilizowekwa na mamlaka hiyo wananchi hawapaswi kuwapa kazi ya kufunga umeme kwenye nyumba zao na viwanda kwa mafundi ambao hawana leseni ya mamlaka hiyo.