CARACAS, VENEZUELA
RAIS wa Venezuela, Nicolas Maduro amemwandikia barua Kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani, Papa Francis akimwomba aingilie kati mgogoro wa kisiasa unaoendelea hapa.
“Nimemwandikia barua Papa Francis”, alisema Maduro wakati akizungumza na Kituo cha Habari cha Italia cha SkyTg24.
Amesema amemwomba kusaidia kufanikisha mchakato wa majadiliano, akigusia juhudi kama hizo zinazofanywa na mataifa ya Mexico, Uruguay, Bolivia na mataifa mengine.
“Nimemuomba Papa kutusaidia, kwenye mchakato wa majadiliano. Ninatumaini tutapata majibu ya kutia moyo kutoka kwake”, alisema Maduro.
Waziri Mkuu wa Japan Shinzo Abe na Kansela wa Ujerumani Angela Merkel kwa pamoja wamesema wana matumaini ya ufumbuzi wa amani kwenye mgogoro huo wa kisiasa.
Aidha Merkel amesema taifa lake linamtambua kiongozi wa upinzani, Juan Guaido aliyejitangazia mwenyewe kuwa rais wa mpito.
Abe, hata hivyo hakutoa msimamo juu ya Guaido, lakini alisema Japan inataka suluhisho la amani na demokrasia kwenye mgogoro huo.