26.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Maduka ya kubadilishia fedha yaliyofungwa sasa kufunguliwa kwa kibali maalumu

JANETH MUSHI-ARUSHA

SERIKALI imesema inamalizia kuandaa utaratibu kupitia Benki Kuu (BoT), ikiwemo uhakiki wa taarifa za maduka ya kubadilishia fedha za kigeni yaliyofungiwa ili kuweza kutoa vibali maalumu kwa maduka hayo kuendelea na biashara hiyo.

Pia imesisitiza utawala bora katika taasisi za kifedha ikiwemo benki kwani ndiyo msingi wa maendeleo na katika kipindi cha mwaka jana benki tano zilifungwa baada ya kufilisika na kusababisha hasara kwa wateja, wawekezaji, wadau mbalimbali na wanahisa.

Kauli hiyo ilitolewa jana jijini hapa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, alipokuwa akifungua semina ya wanahisa wa Benki ya CRDB, iliyofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa AICC, kabla ya kufanyika kwa mkutano mkuu wa 24 unaotarajiwa kufanyika leo.

Alisema Serikali imefanya jitihada za kuratibu mfumo wa udhibiti wa matumizi ya fedha za kigeni unaolenga kuondoa biashara ya dola kiholela na kuwa wameanza na benki kupata vibali vya kubadili fedha za kigeni na kuwa baada ya uhakiki watatoa fursa kwa wafanyabiashara mmoja mmoja wa maeneo mbalimbali ya kimkakati nchini.

“Tumeanza na mabenki baada ya uhakiki unaoendelea tunaweza tukatoa fursa kwa wafanyabiashara mmoja mmoja wa maeneo ya kimkakati ili kuwa na maduka tunayoyafahamu, yaliyosajiliwa vizuri yanayoweza kufanya biashara hii vizuri kuliko ambavyo ilikuwa awali.

“Niseme hata kwa wale ambao walikuwa wanafanya biashara hiyo na shughuli zao kwa sasa zimesimama, BoT inakamilisha uratibu wao na mawasiliano yao na wateja wao ili baadaye kwa utaratibu mzuri wa kutoa vibali vya uendeshaji wa maduka hayo kwa hiyo wale wote ambao walikuwa na maduka wasiwe na mashaka taratibu zinaendelea.

“Lakini kwa sasa CRDB ni miongoni mwa benki na inaongoza kufanya biashara ya kubadili fedha, nawapongeza kwa mikakati mbalimbali mnayoweka ikiwemo ya kushiriki shughuli ambazo Serikali yetu inafanya na yanayoleta tija kiukweli mmetufikisha pazuri,” alisema.

Akizungumzia kuhusu utawala bora katika taasisi za fedha, alisema suala hilo limekuwa likizungumzwa katika vyumba vya mikutano bila kutekelezwa, vitendo vinavyochangia mashirika mengi ya umma na binafsi kufilisiwa.

“Mwaka mmoja uliopita tulifungia benki tano ambazo zimefilisika hazina uwezo wa kujiendesha, lakini wateja wameweka fedha zao kule ndani na wateja wanatarajia warudishiwe fedha zao, haziko ndani ya benki kwanini kwa sababu ya kukosa utawala bora,” alisema na kuongeza:

“Ambapo watendaji kazi yao ni  kuchomoa chomoa fedha kutoratibu vizuri na leo hii tunashuhudia Watanzania wenzetu waliokuwa wameweka fedha zao kule wakiwa wamepata hasara, hatutarajii kwa benki yetu ya CRDB  kwa mifumo iliyojiwekea kwa safu nzuri ya utawala inayoongoza benki hii ifike huko, tunaamini benki hii itaendelea kuwa mfano wa benki nyingine nchini.”

Waziri Mkuu aliipongeza benki hiyo kwa ufanisi na utendaji kazi wake na kuitaka kupitia kitengo chake cha elimu kwa wateja kutoa elimu ya mikopo na namna ya kuitumia kwani wananchi wengi wamekuwa wakilalamika kuuziwa mali zao walizoweka dhamana baada ya kushindwa kuilipa kutokana na kukosa elimu ya mikopo.

Aidha, alitumia fursa hiyo kusisitiza uwajibikaji mahali pa kazi kwa viongozi na watendaji katika sekta mbalimbali, utawala wa sheria katika kila sekta na ushirikishwaji wa wadau.

Mwenyekiti wa Bodi ya CRDB, Ally Laay, alisema imetoa gawio la asilimia 35 kwa Serikali ambayo ni sawa na Sh bilioni 19.5, zitakazochangia kutunisha mfuko wa taifa na kuwa wataendelea kutoa gawio ili kuboresha huduma mbalimbali.

Aidha, alisema Watanzania wengi hawajui umuhimu wa kuwekeza katika hisa hivyo elimu zaidi inahitajika kwa jamii.

“Watanzania tujenge tabia ya kuwekeza katika hisa na elimu hii tuhamasishe jamii zaidi wawekeze kwenye hisa kwani wengi hawaamini kuwekeza katika hisa na badala yake wanawekeza katika magari, nyumba na mashamba, ufahamu ni mdogo katika hili kwenye mitaala masuala ya hisa tuweke ili watoto wetu wabadili mtazamo,” alisema.

Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB, Abdulmajid Nsekela, alisema semina hiyo imekutanisha wanahisa zaidi ya 29,000.

Kwa upande wake Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato nchini (TRA), Charles Kachere, aliiomba Benki ya CRDB kwa kushirikiana na taasisi nyingine za fedha kutoa elimu kwa jamii ya kuhamasisha wananchi wawekeze katika hisa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles