27.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Madereva watakiwa kuzingatia sheria kuokoa maisha ya watoto

NA MWANDISHI WETU

-DAR ES SALAAM

MADEREVA wametakiwa kuzingatia sheria za usalama barabarani ili kuokoa maisha ya watoto kutokana na vifo vingi kusababishwa na uzembe.

Kauli hiyo ilitolewa Dar es Salaam jana na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Puma Energy Tanzania, Dominic Dhanah, wakati wa maadhimisho ya Wiki ya Kimataifa ya Nenda kwa Usalama Barabarani (UN-Global Road Safety Week (UNGRSW)) na kuwatumia wanafunzi wa Shule ya Msingi Bunge ya Dar es Salaam kutoa elimu kwa madereva.

 “Tumeamua kuwatumia watoto, lengo ni kuhakikisha wanaanza kupata uelewa kuhusu masuala ya usalama barabarani. Tupo nao kwa sababu hawa ni mabalozi wetu. 

“Vilevile tunatoa elimu kwa wateja wetu namna ya kutumia barabara ili kulinda maisha,” alisema Dhanah.

Meneja Programu ya Usalama Barabarani wa Puma Energy, Neema Swai, alisema kaulimbiu ya mwaka huu ni “sema usikike na okoa maisha”.

Alisema wanatoa elimu kwa watoto na wanawatumia kuwaelimisha madereva kwa kuwa ndio wahanga wakubwa wa vifo vitokanavyo na uzembe barabarani.

“Kila siku watoto ndio wanaotumia barabara kwenda shule na kurudi nyumbani, wasipokuwa na elimu ya kutosha tutawapoteza wengi,” alisema na kuongeza:

“Mtambue, kwa mujibu wa takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO), watoto wenye umri kati ya miaka mitano hadi 29, wanapoteza maisha kwa wingi kutokana na ajali na si malaria wala ugonjwa mwingine bali ni ajali.

 “Serikali inatumia gharama kubwa kumtunza mtoto kuanzia miaka 0-5 halafu anakuja kufa kwa ajali ya barabarani kutokana na uzembe wa madereva au kukosa elimu ya usalama barabarani, hilo tumelikataa ndiyo maana tunasema tumeamua kupaza sauti.”

Mmoja wa wanafunzi walioshiriki kutoa elimu, Godbless Mlacha, anayesoma darasa la sita katika Shule ya Msingi Bunge, alisema wanawaasa madereva kuacha kutumia vilevi au kuendesha kwa mwendo kasi wakiwa barabarani kwa kuwa maisha yao yanakuwa hatarini.

 “Nahitaji kuishi ili nitimize ndoto zangu, uzembe wa dereva unaweza kuondoa uhai wangu au kunipa kilema cha kudumu. Nimechagua kupaza sauti ili kumaliza hili tatizo,” alisema Mlacha.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles