23.3 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Madereva wabuni mbinu mpya ya mgomo

NA CHRISTINA GAULUHANGA, DAR ES SALAAM

CHAMA cha Madereva Wafanyakazi Tanzania (TADWU), kimesema madereva nchi nzima watakuwa mapumziko kwa wiki moja au zaidi kwa ajili ya kujiunga na mafunzo ya udereva.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Katibu wa TADWU, Rashid Said, alisema baada ya mazungumzo na Kamati ya Kudumu ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, wameshindwa kuafikiana na kuona kuwa matajiri ndiyo wana nguvu zaidi kuliko wao waajiriwa.

Alisema kutokana na hali hiyo wameamua kutoendelea na mgomo na badala yake kuanzia Agosti 19 (Jumatano), hadi 24, mwaka huu watakuwa na mafunzo ya udereva nchi nzima.

“Tumeona suala la shinikizo la migomo halina matunda kwetu na kwa vile mazungumzo na Serikali yamekwama, tumeamua kutumia mtindo mpya wa kupiga kwa kutumia bunduki kubwa…tutaingia mafunzoni kwa wiki moja au zaidi madereva wote,” alisema Said.

Alisema anaamini njia hiyo mpya itasaidia kupambana na maadui ambao ni waajiri wao wanaowanyima haki zao za msingi.

“Kwa kuwa hatujaridhika na maamuzi yaliyofikiwa katika kikao cha mwisho cha upatanishi chini ya kamati ya Waziri Pinda, tumebaini hakuna urafiki wa kudumu kati ya tajiri na masikini,” alisema.

Aliongeza kuwa hawawezi kucheka na waajiri ikiwa yaliyopiganiwa hayajatekelezwa, watahakikisha  wanaendelea kupambana japokuwa wanaopambana nao ni vigogo.

“Sisi kama chama tunafuata maelekezo ya wanasheria wetu ambao wamewaeleza wasigome wafuate sheria na hawatagoma bali watakuwa na mafunzo nchi nzima,” alisema.

Alisema mafunzo hayo yatafanyika kwa kanda nchi nzima, Pwani itakuwa ni Dar es Salaam, Kaskazini Arusha na Kusini (Mtwara).

Pia aliongeza madereva wote wa Kanda ya Ziwa watahudhuria mafunzo hayo Mwanza na Kanda ya Juu, Mbeya hivyo wananchi wawe wavumilivu kipindi chote cha mafunzo kwa kuwa yanalenga kuokoa maisha yao katika kupunguza ajali.

Said alisisitiza kuwa madereva wameburuzwa na kunyanyaswa vya kutosha na waajiri wao hivyo sasa ni muda wa ukombozi kwa kusikilizwa matakwa yao kwa kuwa mgogoro uliopo kati ya madereva na wamiliki ni mkubwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles