28.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

MADEREVA 63 MBARONI KWA KUTOVAA KOFIA NGUMU

CHRISTINA GAULUHANGA NA FERDNANDA MBAMILA-DAR ES SALAAM

JUMLA ya madereva 63 wa pikipiki maarufu bodaboda, wamekamatwa na Kikosi cha Usalama Barabarani nchini kwa makosa mbalimbali ikiwamo kutovaa kofia ngumu (helmet) na kupita katika barabara zisizoruhusiwa.

Akizungumza na MTANZANIA ofisini kwake, Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani nchini, Mohamed Mpinga, amesema madereva hao walikamatwa katika operesheni maalumu ya kuwasaka madereva wa pikipiki wanaovunja sheria ikiwamo kupita kwenye barabara za mabasi yaendayo haraka (Dart).

“Madereva hawa baadhi yao wanaendelea kushikiliwa na polisi huku wengine wakiwa nje baada ya kutimiza masharti ya dhamana ambapo leo watafikishwa mahakamani kujibu mashtaka yao,” alisema Mpinga.

Aidha, alisema operesheni ya kuwakamata madereva wa pikipiki na magari wanaokiuka sheria ilianza mapema wiki hii na ni endelevu ambapo pia wamefanikiwa kukamata pikipiki 16 na kuzifungua matairi kwa sababu ya kupita kwenye miundombinu ya Dart.

Kamanda Mpinga alisema ukamataji wa magari yenye taa kubwa yameleta matokeo mazuri ambapo hivi sasa wengi wametekeleza agizo la kuziondoa taa hizo.

Naye Mjumbe wa Kamati ya Bodaboda Mkoa wa Dar es Salaam, Abdallah Bakari ambaye pia ni msemaji wa bodaboda, amewataka madereva wa pikipiki kuzingatia sheria za usalama barabarani.

Alisema ni vyema wakatii sheria bila shuruti kwa sababu Jeshi la Polisi tayari limeanza kutoa adhabu.

“Kwa sasa trafiki wamekuwa wakali mara mbili ya tulivyowazoea hivyo ni vyema wenzangu waendesha pikipiki wakazingatia sheria,” alisema Bakari.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles