30.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Maambukizi ya corona yapindukia milioni 16

 BRUSSELS, UBELGIJI

IDADI ya maambukizi ya virusi vya Corona kote duniani imepindukia milioni 16 kufikia jana, Jumapili Julai 26, 2020.

Kwa mujibu wa takwimu za shirika la habari la AFP, zaidi ya nusu ya maambukizi hayo yameripotiwa katika bara la Amerika na nchi za Carribean.

Katika idadi hiyo iliyotajwa, zaidi ya watu 600,000 wamefariki dunia huku Marekani ikiongoza kwa maambukizi ya virusi vya corona duniani.

Nchini Marekani zaidi ya watu milioni nne wamethibitishwa kuwa wameambukizwa virusi vya corona na watu 146,460 wamefariki dunia.

Huko Amerika ya Kusini na nchi za Carribean zaidi ya watu milioni nne wameambukizwa na 182,501 wamefariki dunia kutokana na ugonjwa wa Covid-19 unaosababishw ana virusi hivyo vya corona. 

Bara Ulaya limeorodhesha maambukizi zaidi ya milioni tatu na watu zaidi ya 200,000 wamefariki dunia.

Shirika la Afya Duniani (WHO) lilisema maambukizi yanaendelea kuenea kwa kasi duniani kote.

Katika hatua nyingine, watalii raia wa Uingereza wanaorudi nchini mwao kutoka Hispania wamekasirishwa na uamuzi wa ghafla wa serikali yao kuwalazimisha kukaa karantini kwa muda wa siku 14.

 Uamuzi wa Uingereza kuiondoa Uhispania katika orodha ya nchi salama ulitangazwa juzi Jumamosi, na kuwaacha njia panda wasafiri wanaoingia Uingereza.

Utawala wa Waziri Mkuu, Boris Johnson umekosolewa vikali kwa uamuzi huo ambao umechukuliwa baada ya idadi ya maambukizi ya virusi vya Corona kupanda nchini Uhispania.

Hispania ilikuwa kwenye orodha ya nchi salama, hatua hiyo ikimaanisha kuwa sio lazima kwa wasafiri wanaotokea nchini humo na kuingia Uingereza kukaa karantini.

Hata hivyo kufuatia ongezeko la maambukizi ya Covid-19 nchini humo, imelazimu baadhi ya miji kama vile Barcelona kuweka tena sheria za kuwalazimu watu kuvaa barakoa na kuwataka watu kusalia majumbani.

Huko Korea Kaskazini, Kiongozi wa nchi hiyo, Kim Jong Un ametangaza hali ya dharura pamoja na kuweka vizuizi katika mji wa mpakani wa Kaesong baada ya mtu mmoja kudhaniwa kuwa na virusi vya corona.

Chombo cha habari cha serikali KCNA kimeripoti kuwa mtu huyo alivuka mpaka kwa njia isiyo halali akitokea Korea Kusini.

Shirika la habari la serikali limeripoti kuwa mtu huyo anayedhaniwa kuwa ameambukizwa virusi vya corona aliiasi Korea Kaskazini miaka mitatu iliyopita na kukimbilia Korea Kusini.

Taarifa zilisema kwamba alivuka mpaka wa Kaesong kinyume cha sheria Julai 19, 2020 na kuingia nchini Korea Kaskazini akiwa na dalili za virusi vya corona vinavyosababisha ugonjwa wa Covid-19.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles