23.3 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

MAALIM SEIF AMSHTAKI LIPUMBA KWA GWAJIMA

Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad (kushoto), akizungumza na Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima kanisani kwake Ubungo, Dar es Salaam jana. Picha na Jumanne Juma

 

 

Na ASHA BANI-DAR ES SALAAM

KATIBU Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharrif Hamad, amemshtaki Mwenyekiti anayetambuliwa na Msajili wa Vyama vya Siasa, Profesa Ibrahimu Lipumba kwa Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima , Josephat Gwajima.

Maalim Seif jana alikwenda katika Kanisa la Askofu Gwajima saa 10 jioni na kuteta kwa takribani saa moja na baadaye kuzungumza na waandishi wa habari waliokuwa nje ya jengo la kanisa hilo lililopo Ubungo jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na waandishi wa habari ambao walitaka kujua sababu za yeye kufika kanisani hapo, Maalim Seif alisema alikwenda kufanya mazungumzo na kumweleza mambo mbalimbali likiwemo suala la mgogoro unaofukuta kwa sasa ndani ya CUF.

Alisema Askofu Gwajima ni rafiki yake na kwamba  hawajaonana siku nyingi lakini pia kiongozi huyo  alikuwa haelewi chanzo kilichosababisha mgogoro huo na nani aliyeusababisha.

“Nimemweleza mgogoro wote uliopo ndani ya CUF na ninaamini Askofu Gwajima ataamua mwenyewe nini afanye kutokana na niliyomweleza.

“Mbali na Askofu Gwajima pia nimefanya mazungumzo na viongozi mbalimbali wa kidini wakiwamo wa kiislamu na lengo kubwa kuueleza kinachoendelea ndani ya chama chetu,” alisema Maalim Seif.

Kwa upande wake Askofu Gwajima, alisema anajipanga kumlipua Profesa Lipumba siku ya Jumapili kanisani hapo lakini baada ya kumaliza kufanya uchunguzi wa suala hilo.

“Maalim Seif ni rafiki yangu wa siku nyingi lakini Lipumba sina urafiki naye na hivyo siwezi kukaa naye kuzungumza naye lolote kwa kuwa bora kuzungumza na rafiki yangu huyo kuliko mtu ambaye si rafiki yangu,” alisema Gwajima.

Alipoulizwa kuwa watu watarajie Jumapili kwenye ibada alijibu. “ Enheee! kumbe mnajua hivyo subirini Jumapili,” alisistiza Askofu Gwajima.

Mgogoro unaokitafuta sasa chama cha CUF unatokana na kila upande kushikilia msimamo wake huku Maalim Seif akististiza kuwa Lipumba si Mwenyekiti wala mwanachama wa chama hicho.

Siku chache baadaye Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, Jaji Francis Mutungi, alitoa tafsiri ya Katiba ya CUF na kupinga maamuzi ya Mkutano Mkuu wa chama hicho huku akisistiza Lipumba ni Mwenyekiti halali wa CUF.

Agosti 21, 2015 Profesa Lipumba alitangaza kujiuzulu uenyekiti ndani ya chama hicho cha CUF baada ya kuibukia kwa sintofahamu ndani ya chama hicho.

Juni 13, 2016 Profesa Lipumba, alitangaza kusudio la kuondoa barua yake ya kujiuzulu na kukataa kurejea kwenye nafasi yake ya uenyekiti, jambo ambalo lilizua mjadala mzito ndani ya chama hicho.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles