Na Mwandishi Wetu
Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limesema kuanzia Februari 18 hadi 22,2025 limewakamata watuhumiwa 26 kwa tuhuma za kujihusisha na biashara haramu ya upatu mtandaoni bila kuwa na kibali kutoka Benki Kuu Tanzania.
Taarifa iliyotolewa na Polisi leo Februari 24,2025, imewataja baadhi ya watuhumiwa hao kuwa ni Najim Issa Houmud Mkurugenzi (34) mkazi wa Kigamboni, Hatibu Kudura (25) mkazi wa Kinondoni, Fatum Hamisi (26) mkazi wa Kigamboni na Athumani Sadik (29) mkazi wa Mabibo.
Taarifa hiyo imesema watuhumiwa hao walikamatwa katika maeneo ya Mbagala, Gongolamboto, Tabata, Mbezi Magufuli, Ubungo Riverside na Mabibo ambapo Jeshi la Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam kwa kushirikiana na Benki Kuu ya Tanzania lilifanya uchunguzi wa kampuni ya LEO BURNETT LONDON (LBL) inayo jihusisha na biashara ya upatu mtandaoni na kubaini kuwa kampuni hiyo haina uongozi maalum.
Vilevile limebaini ufanyaji kazi wake ili uweze kujiunga ni lazima utoe kiasi cha pesa kuanzia sh 50,000 na kuendelea ili uwe mwanachama, pia huchangisha pesa kwa kuwadanganya wananchi kuwa watapata faida kubwa kwa muda mfupi bila ya wanachama kuhusishwa kwa namna yoyote katika shughuli za uendeshaji wa kampuni hiyo.
“Mara upelelezi utakapokamilika watuhumiwa wote watafikishwa Mahakamani kujibu tuhuma
zinazowakabili, Jeshi la Polisi linatoa wito kwa Wananchi wote kuacha kujihusisha na biashara za upatu mitandaoni bila kujiridhisha kwanza kwa kuwa baadhi ya biashara hizo hazina leseni wala vibali kutoka Mamlaka za kisheria zinazohusika hivyo kuhatarisha usalama pesa zao,” imesema taarifa hiyo.