25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Lugola aagiza kuhamishwa askari wote kituo cha polisi

Walter Mguluchuma-Katavi

WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, ametoa siku saba kwa Polisi Mkoa wa Katavi kuwahamisha askari wote wa Kituo cha Polisi Majimoto.

Lugola alitoa agizo hilo juzi wakati wa mkutano wa hadhara uliofanyika stendi ya Majimoto wilayani Mlele mkoani Katavi, wakati akijibu kero za wananchi.

Alisema kupitia kero zilizowasilishwa na wananchi, zinaonyesha wazi askari 15 wa kituo hicho wanajihusisha na rushwa, kupiga wananchi ovyo wakiwemo bodaboda, kushindwa kudhibiti ulinzi na usalama na kutoshughulikia malalamiko ya wananchi.

“Nataka niseme haya kutoa mfano, ili iwe fundisho kwa wengine kote nchini, Kaimu kamanda, natoa siku saba askari wote wa kituo hiki wahamishwe na waletwe wengine ili wajifunze,” alisema Lugola.

Hata hivyo baada ya agizo hilo, Lugola aliwauliza wananchi kama askari wote wanatakiwa kuhamishwa, ambao walikubali, lakini walipinga mkuu wa kituo hicho Iddy Kombo asihamishwe.

“Asihamishwe, asihamishwe, asihamishwe,” zilisikika sauti za wananchi hao katika mkutano huo.

Lugola alisema Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi imepiga hatua kubwa kwa kupambana na uhalifu, hasa ujambazi, jambo ambalo limeleta matokeo chanya na matukio hayo kupungua kwa kasi nchini.

Aidha Lugola alipiga marufuku askari polisi kuwaweka watuhumiwa mahabusu na kuwanyima dhamana hata kwa wale wenye kesi ndogo.

Aliwataka wananchi kutojihusisha na biashara haramu ya usafirishaji binadamu kwani kufanya hivyo ni kosa kwa mujibu wa sheria za nchi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles