25.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Lowassa: Sitasahau magumu niliyopitia

Pg 1 (2)Na Asifiwe George, Dar es Salaam

ALIYEKUWA mgombea urais wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kwa mwamvuli wa Ukawa, Edward Lowassa  amesema kamwe katika maisha yake, hatasahau mambo mengi magumu aliyoyapitia.

Amesema pamoja na changamoto zote alizopitia, bado Mungu ameweza kumsimamia hadi akavuka salama vikwazo vyote.

Amesisitiza kuwa hajakata tamaa na ataendelea kuwatumikia Watanzania kwa moyo wake wote.

Lowassa alitoa kauli hiyo nyumbani kwake Masaki   Dar es Salaam jana,  saa chache baada ya Ibada Maalum ya shukrani iliyofanyika katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Mashariki na Pwani, Azania Front.

Lowassa ambaye pia ni Waziri  Mkuu wa zamani, alisema alipitia mambo mengi yakiwamo ya Uchaguzi Mkuu uliofanyika mwaka jana, lakini Mungu alimsaidia na kumtia moyo.

“Kutokana na magumu mengi niliyopitia sina budi kutoa shukrani mbele za Mungu. Nilikuwa ninaisubiria sana siku kama ya leo ili mimi na familia yangu  tutoe shukrani mbele ya Mungu tena kanisani na leo nimetimiza ahadi yangu si kwa uwezo wetu bali ni kwa neema ya Mungu.

“Wapo Watanzania wengi walioguswa  kwa ajili yetu wakiwamo wachungaji, maaskofu, mapadri na viongozi wa siasa.

“Wote hawa walituwezesha sisi kama familia kufikia hapa kwa michango yao ikiwa ni pamoja na maombi  hivyo niliona ni vema nijumuike nao katika hafla hii fupi ya shukrani,” alisema Lowassa.

Lowassa  alisisitiza kuwa  Mungu ndiye kiongozi katika maisha yake hivyo anaamini ataendelea kumwongoza  aendelee kuwatumikia Watanzania kwa moyo wake wote.

Awali akiwa kanisani baada ya kumalizika ibada hiyo, Lowassa aliwataka Watanzania kusherehekea Sikukuu ya Pasaka kwa amani.

“Sikukuu kama hii tunapaswa kuitumia kuendelea kuhubiri amani ya nchi yetu…pia tukumbuke suala la Zanzibar ambalo limekuwa likikwamisha baadhi ya michakato ya maendeleo,”alisema mwanasiasa huyo mwenye ushawishi mkubwa katika jamii.

Mbowe aiangukia familia ya Lowassa

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe aliiomba familia ya mwanasiasa huyo kumruhusu Lowassa  aendelee kuwatumikia wananchi.

Alisema mabadiliko aliyoyafanya Lowassa baada ya kuhamia vyama vya upinzani kabla ya kuanza   kampeni Agosti mwaka jana, ni makubwa na yameleta nuru ya matumaini kwa Watanzania.

Mbowe ambaye pia ni Mbunge wa Hai na Kiongozi wa Kambi ya Upinzania Bungeni, alisema kwa muda mrefu Watanzania walihitaji mabadiliko ya fikra na matendo  lakini baadhi yao walikuwa wakiyaongoza kwa woga.

Mbowe alisema uchaguzi si tukio bali ni sehemu ya mchakato na kwamba kama kuna mtu aliyeangalia uchaguzi kama tukio atakuwa amekata tamaa.

“Tuna wajibu wa kuendeleza kazi aliyoifanya  Lowassa, tunatambua wananchi walipigana sana kwa ajili ya kufanya mabadiliko na Lowassa alikuwa mshika bendera.

“Sasa kila mmoja kwa nafasi yake awe ndani au nje ya chama  ana wajibu wa kuendeleza alichokifanya Lowassa.

“Niipongeze familia hii kwa uamuzi wenu mliouchukua  wa kwenda kanisani kumshukuru Mungu kutokana na changamoto mbalimbali zilizojitokeza.

“Hiki mlichokifanya kwa familia, marafiki na taifa kwa ujumla ni jambo la heri na linafaa kuigwa,” alisema Mbowe.

Askofu Lwiza

Awali akizungumza baada ya Ibada ya Jumatatu ya Pasaka katika Kanisa la Azania Front, Mchungaji Msaidizi wa Kanisa hilo, Chediel Lwiza alisema hatua ya baadhi ya maaskofu na viongozi wengine kumuunga mkono Lowassa wakati wa uchaguzi si dhambi na ni suala la utashi.

Alisema maaskofu na watu wengine wakitangaza kumuunga mkono mwanasiasa kwa jambo lolote ni sawa  kwa sababu kuna njia ya siasa na roho.

“Hakuna dhambi yoyote iliyotendeka kwa Askofu kutangaza kumuunga mkono Lowassa katika siasa, ni haki yake kwa vile  Katiba inamruhusu. Pia hata akimuunga mkono katika roho na katiba bado ana haki,”alisema.

Mchungaji huyo alizungumzia kasi ya Rais John Magufuli akisema rais anatakiwa kusaidiwa kazi ya utumbuaji majipu ili asichoke.

“Rais anatakiwa asaidiwe kazi anayoifanya kwa sasa kwa sababu  ni nzito sana, hivyo endapo akiachiwa peke yake atachoka ndani ya kipindi kifupi,”alisema.

Alisema kitendo cha Magufuli kusimamia misingi ya haki hana budi atambue kuwa lazima atakuwa na maadui kila sehemu.

“Rais Magufuli anaposema aombewe ni kwa sababu anakutana na chuki za baadhi ya watendaji ambao hawapendezwi na msimamo alionao,”alisema.

Askofu Malasusa

Naye Askofu Mkuu wa KKKT Dayosisi ya Mashariki na Pwani, Dk. Alex Malasusa alisema mfululizo wa viongozi kanisani hapo ni ishara ya umoja na amani kwa kuwa wote ni wakristo.

“Nashukuru kwa wale wote waliokuja kusali kanisani hapa ingawa si waumini wa kanisa hili, lakini kutokana na tukio la leo (jana) ndiyo maana wamefika.

“Ni ishara njema kwa kanisa hili kwa vile  leo hii…kuna wengine waliokuja ni waislamu lakini wamevutika na idadi ya viongozi wa Ukawa waliofika,’alisema Askofu Malasusa.

Alisema   anawapongeza kufika kanisani hapo kama viongozi wa  siasa wenye ucha Mungu na kanisa linajivunia kuwa na viongozi wa namna hiyo.

Askofu Mameo

Akitoa mawazo yake, Askofu wa (KKKT) Dayosisi ya Morogoro, Paul ole Mameo alisema alifika kanisani hapo  kumsindikiza Lowassa ambaye alienda kutoa shukrani ya pekee kwa yote aliyotendewa na Mungu.

Mameo alisema kila mtu anapaswa kumshukuru Mungu kwa kila jambo na   kitendo alichokifanya Lowassa kiwahamasishe na wengine kujenga mazoea ya kutoa shukrani za pekee kwa Mungu.

“Nimekuja hapa kumsindikiza Lowassa, kitendo alichokifanya kinapaswa kuigwa na kila mmoja wetu, mimi mwaka jana nilifanya kama hivi….hivyo nawashauri wenzangu nanyi muige mfano huu.

“Mungu wetu ni wa rehema na anamtendea wema kila mmoja wetu hivyo anapaswa kutolewa shukrani.

“Angalia kuna ajali zinatokea watu wanakatika miguu, wengine wako hospitalini lakini sisi tupo wazima, Mungu anaendelea kutupigania,” alisema Askofu Mameo.

Alisema imekuwa ni bahati ya pekee kwa watu wenye umaarufu na utashi wa siasa kumkumbuka Mungu kwa yale aliyoyatenda. 

Meya Mwita

Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Isaya Mwita ambaye pia alihudhuria ibada hiyo na kutambulishwa kwa waumini wa kanisa hilo,   aliwashukuru wananchi wa Dar es Salaam kwa kuiamini Ukawa na kuipa nafasi.

Mbali na familia ya Lowassa pia ibada na hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa dini na siasa wakiwamo  Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia, Meya wa Kiondoni, Boniface Jacob na Meya wa Ilala, Charles Kuyeko.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles