24.7 C
Dar es Salaam
Tuesday, March 19, 2024

Contact us: [email protected]

Lowassa: Ipo siku nitaingia Ikulu

8qsPaAk9NA ELIYA MBONEA, ARUSHA

ALIYEKUWA mgombea urais kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na kuungwa mkono  Ukawa, Edward Lowassa amesema ipo siku ataingia katika Ikulu  kwa kupigiwa kura na Watanzania.

Lowassa alitoa kauli   mjini hapa jana katika Viwanja vya Shule ya Msingi Sinoni wakati akimuombea kura mgombea ubunge wa   Arusha Mjini, Godbless Lema.

Akizungumza kwa mara ya kwanza tangu matokeo ya urais yalipotangazwa na kumpa ushindi Dk. John Magufuli, Lowassa alisema anaamini kwamba Watanzania ambao kura zao ziliibwa ndiyo watakaompeleka Ikulu kwa vile  bado yupo imara.

Alisema baada ya kutangazwa   matokeo wapo baadhi ya viongozi na wafuasi wa Chama hicho waliomtaka atoe kauli kuhusiana na dhuluma aliyofanyiwa ya kuibiwa kura zake lakini aliwaambia hakuwa tayari kuingia Ikulu yenye mikono ya damu za Watanzania.

“Ni mara yangu kwanza kusimama mbele yenu tangu tulipomaliza uchaguzi mkuu.  Naomba niwaambie nawapenda sana Watanzania sihitaji kuingia Ikulu kwa damu ya watu. Naamini Watanzania hawa hawa watanipeleka Ikulu siku moja, bado nipo imara.

“Hawa CCM na Serikali yao wamechakachua kura zetu, dunia inajua. Naomba niwahakikishieni tumeshinda Uchaguzi Mkuu, sisi ndiyo washindi hata wao wanajua. Tembeeni kifua mbele sisi ni washindi,” alisema Lowassa huku akishangiliwa kwa kauli mbiu za ‘Lowassa mabadiliko’, ‘Mabadiliko Lowassa’ na kuongeza:

 

“Nawaomba sana mchagueni Lema kwani mkishamchagua mtakuwa mmezidi kuniimarisha. Kwani ninaamini ukiwatuma Lema na mgombea yule wa CCM hakika Lema atamshinda kwa mbali.”

 

Akifafanua kuhusu hoja walizokuwa wakisema   wakati wa kampeni, Lowassa aliishukuru Serikali kwa kumwachia Sheikh Ponda na  aliiomba Serikali  kufanya hivyo hivyo kwa mwanamuziki Nguza Viking na mwanaye.

“Haya mambo ndiyo tuliyoyasema wakati wa kampeni, sasa Magufuli ameanza kuyatekeleza. Sasa namuomba angalau wawe wanasema hizo ni sera za Lowassa na CHADEMA na wanapozitumia basi wawe wanatushukuru,” alisema Lowassa na kushangiliwa.

 

Huku akimnadi   Lema, Lowassa aliwaomba wananchi hao wa   Arusha kutomchagua mgombea anayesambaza ukabila kwa kutanguliza kabila lake mbele ya wananchi.

“Mtu anayekuja kuomba kura kwa kujitambulisha yeye ni kabila fulani mwambieni hapa hatutamtambua bali tunachagua mbunge kwa ajili ya maendeleo,” alisema Lowassa.

Lowassa aliyekuwa mwenye furaha zaidi aliwaambia wananchi hao kutohangaika na magari ya maji ya kuwasha ya polisi kwani serikali inatafuta mahali pa kuonyesha uhalali kuwa magari hayo baada ya kuagizwa yalitumika.

Alisema   Dola za Marekani milioni 200 zilitolewa na Serikali ya Awamu ya Nne kwa ajili ya kununua magari hayo ya polisi.

“Ndugu zangu msiwape sababu kuwa magari yao yalitumika endeleeni kuwapuuza,” alisema.

Naye Waziri  Mkuu wa zamani Frederick Sumaye ambaye aliihama CCM kabla ya   Uchaguzi Mkuu na kiujunga na UKAWA,   alisema majipu ya CCM yanayotumbuliwa na Rais Dk. Magufuli   yaliyoungana na mishipa ya damu inayopeleka damu kwenye moyo.

“Dhuluma iliyowahi kufanywa na Serikali na CCM ni kubwa mno kwa watanzania. Hiki kinachofanyika sasa ndicho tulichokipigia kelele kwenye kampeni wengine wakatutukana na kutuita majina ya ajabu.

“Sasa leo ndiyo tunaona Magufuli ameanza kutekeleza yale tuliyokuwa tukiyapigia kelele  wakati ya kwao hakuna hata moja walilotekeleza,” alisema Sumaye na kuongeza:

“Wananchi wa Arusha nawaomba sana mnichagulie Lema   aweze kwenda kuungana na wabunge wenzake kwa ajili ya kutumbua majipu yanayopeleka damu kwenye mishipa ya damu kwani majipu hayo Magufuli na wenzake hawawezi kuyatupumbua.”

Naye  aliwapongeza wakazi wa Arusha kwa kuwa kielelezo cha mabadiliko nchini na aliwaomba kuhakikisha heshima ya mabadiliko hiyo wanazidi kuipeleka kwa Lowassa.

Akizugumza kuhusu upigaji wa kura na kutangazwa matokeo, Lema alionya vitendo vya wizi kwa CCM na Serikali akisisitiza kuwa kufanyika kwa vitendo hivyo kutaleta madhara makubwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
584,000SubscribersSubscribe

Latest Articles