27.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 16, 2024

Contact us: [email protected]

Lowassa atikisa makao makuu ya CCM

  • MTZ jmosi new.inddLissu, Sumaye, Mnyika wamshambulia Warioba kwa unafiki

NA MAREGESI PAUL, DODOMA

MGOMBEA urais wa Chama cha Demokarsia na Maendeleo (Chadema) anayeungwa mkono na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Edward Lowassa, jana alitikisa mji wa Dodoma ambao ni Makao Makuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM).

Tukio hilo lilitokea wakati wa mkutano wa kampeni za urais za mgombea huyo ambapo maelfu ya wananchi wa Dodoma walihudhuria mkutano huo uliofanyika katika Viwanja vya Barafu mjini hapa.

Kabla ya mkutano huo, wananchi walianza kujaa uwanjani hapo mapema asubuhi wakiwahi nafasi za kukaa ili waweze kumuona vizuri Lowassa atakapokuwa akihutubia.

Pamoja na hayo, baada ya Lowassa kuwasili uwanjani hapo saa za jioni akiongozana na maofisa kadhaa za Ukawa akiwamo Waziri Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye, kelele za shangwe na vifijo zililipuka kuonyesha ni kwa jinsi gani wanavyomuunga mkono mgombea urais huyo.

Kutokana na hali hiyo, hata alipoanza kuwaomba kura wananchi hao, mara kadhaa alikuwa akilazimika kukatisha hotuba yake kutokana na kelele za shangwe zilizokuwa zikisikika uwanjani hapo.

Pia alisema hakutarajia kupata mapokezi makubwa ya aina hiyo kwa kuwa Mkoa wa Dodoma unadaiwa kuwa ni ngome ya CCM.

Katika maelezo yake, alisema maelfu ya wananchi hao yanamkumbusha idadi kubwa ya wananchi walivyokuwa wakifuatilia mchakato wa wagombea urais wa CCM ambapo jina lake lilikatwa.

“Sikutarajia kupata mapokezi makubwa kiasi hiki na mapokezi haya yananikumbusha kipindi kile cha vikao vya Kamati Kuu na Halmashauri Kuu vya CCM mjini hapa Dodoma.

“Nawakumbuka jinsi Dodoma mlivyojitokeza kusikiliza, nawakumbuka akina mama waliokuwa wakilia kwa ajili yangu, nawakumbuka vijana waliomwagiwa maji na upupu kwa ajili yangu, nawakumbuka wote na nawaambia sasa tunasonga mbele pamoja.

“Nawahakikishia dhamira yangu ya kuwaletea maendeleo bado iko pale pale na nawaahidi nitakapoingia madarakani nyumba ya waziri mkuu itamalizwa haraka iwezekanavyo ili ianze kutumika.

“Nawahakikishia nitaongoza nchi kwa spindi ambayo haijawahi kutokea, haitakuwa nchi ile ile wala ya watu wale wale, itakuwa ni Tanzania mpya,” alisema Lowassa

Kutokana na malengo aliyonayo baada ya kuingia madarakani, aliwataka Watanzania wajiandae kwa maendeleo kwa sababu hatakuwa na muda wa kupoteza

“Jiandaeni, fungeni mikanda kwani safari itaanza Oktoba 25 mwaka huu, nawaambia mnanipa raha na ninataka raha hii muionyeshe siku ya kupiga kura yaani Oktoba 25.

“Wenzetu nao wamejiandaa, lakini sisi tunataka kura kama milioni kumi na ushehe, asanteni sana na Mungu awabariki kwa sababu leo nitalala usingizi mzuri,” alisema Lowassa na kushangiliwa.

Naye Mwanasheria wa Chadema, Tundu Lissu, alisema mwaka huu ni mwaka wa mabadiliko kwa sababu watanzania wamechoshwa na shida walizosababishiwa na CCM.

Pamoja na hayo, Lissu alimshangaa Waziri Mkuu wa zamani, Jaji Joseph Warioba ambaye sasa anakipigia debe CCM licha ya chama hicho kumchafua wakati wa mchakato wa Bunge Maalum la Katiba.

Kwa mujibu wa Lissu, licha ya Jaji Warioba kutukanwa na wana CCM wakati wa mchakato huo wa Katiba, amesahau yote na sasa anawapigia debe ingawa walimdharirisha.

“Sijawahi kumuona Jaji Warioba akiwa amevaa nguo za CCM, lakini jana nilimuona akiwa amezivaa.

“Wote mtakumbuka Jaji Warioba hakushiriki kampeni za 1995, hakushiriki kampeni za 2000, 2005 wala kampeni za 2010, lakini mwaka huu amejitokeza na kusahau yote kwa sababu mtoto wake aitwaye Kipi anagombea ubunge kule Kawe.

“Lakini, nawaomba Watanzania tushirikiane kuiondoa CCM mwaka huu kupitia kwa Lowassa kwa sababu ndiye mwenye uwezo wa kuleta mabadiliko katika nchi hii,” alisema Lissu.

Awali katika mkutano uliofanyika Chamwino, Waziri Mkuu wa zamani, Frederick Sumaye alimshangaa Jaji Warioba  aliyesema wana CCM waliohamia katika vyama vya upinzani wamepungukiwa.

Sumaye alisema kauli ya Jaji Warioba ni kielelezo cha matatizo yalivyojaa CCM.

Kwa mujibu wa Sumaye, baada ya mfumo wa vyama vingi kuanza nchini, kila Mtanzania ana uhuru wa kuhamia chama chochote kwa kuwa anaruhusiwa kufanya hivyo.

“Pamoja na kutukanwa, nawahakikishia katika mikoa mingine CCM wakipata asilimia 20 ya kura, wana bahati.” Alisema Sumaye na kuongeza

Mgombea urais wa CCM, Dk. John Magufuli, hawezi kukomesha rushwa nchini kwa kuwa chama alichomo kina mfumo usiobadilika.

“Kwa hiyo, nawaambia hakuna anayeweza kufanya mabadiliko akiwa CCM, hakuna hata mmoja kwani hata huyo Magufuli aliwahi kukamata meli ya samaki, watuhumiwa wakapelekwa mahakamani, wakashinda kesi na sasa Serikali inatakiwa kuwalipa fidia wenye meli, inatakiwa kulipa samaki waliokamatwa na inatakiwa kulipa riba pia.

“Kwa hiyo, ndugu zangu wana Chamwino, nawaomba msimchague Magufuli, hana lolote atakalolifanya katika nchi hii,” alisema Sumaye.

Mwingine aliyemchambua Warioba, ni mgombea Ubunge wa Kibamba, John Mnyika  ambaye amesema ana sura mbili kutokana na kubadilisha misimamo anayoiamini katika kipindi hiki cha kampeni.

Mnyika ambaye alikuwa akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam alisema tangu kuanza kwa kampeni za Uchaguzi Mkuu kumekuwa na vituko vinavyowalazimu watu kuongea vioja badala ya hoja akiwemo Warioba.

Alisema Warioba anatoa kauli inayoashiria CCM imewafanyia wananchi kazi kubwa huku akisahau katika tume hiyo wamelalamikia kutoridhishwa na mambo yanayofanywa na Serikali katika masuala mbalimbali yakiwemo ya kiuchumi, afya na mengineo huku wengi wao wakitaka  mabadiliko.

Aidha katika mkutano uliofanyika Dodoma mjini aliyekuwa mkuu wa kitengo cha propaganda cha CCM, Tambwe Hiza, aliwataka wasimchague mgombea urais wa CCM, Dk.John Magufuli kwa kuwa ni mbabe, hana huruma na wala hana ubinadamu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles