30.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Lowassa afuta nyayo za Dk. Slaa

Lowassa akihutubiaNa Fredy Azzah, Karatu

MGOMBEA urais wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa, jana aliutikisa Mji wa Karatu wakati akifanya mikutano yake ya kampeni iliyohudhuriwa na maelfu ya wananchi.

Lowassa ambaye anaungwa mkono na vyama vinne vya upinzani ambavyo ni Chadema, NCCR- Mageuzi, Chama cha Wananchi (CUF) na Natonal League for Democracy (NLD) vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) akitumia kauli mbiu yake ya ‘Mabadiliko, Lowassa’ alionekana kuamsha hamasa kubwa ya kisiasa kwa wananchi hao huku baadhi yao wakieleza kuwa amefanikiwa kwa kiwango kikubwa kufunika nyayo za Dk. Willbrod Slaa, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chadema na mbunge wa Karatu kwa kipindi cha miaka 15.

Kabla ya Lowassa kuanza kutoa hotuba katika Uwanja wa Mbowe, Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe, alitumia muda mrefu kuzungumzia safari ya kisiasa na Dk. Slaa ndani ya chama hicho huku akianika sababu za kuondoka kwake kuwa ni shinikizo kutoka kwa mke wake.

 

Mbowe ambaye ni Mwenyekiti Mwenza wa Ukawa, aliyasema hayo jana katika Uwanja huo wenye jina lake la Mbowe ulio Kata ya Karatu wilayani humo.

 

Alisema jana ilikuwa siku yake ya kwanza kuhutubia Karatu baada ya miaka 20 bila kuwa na Dk. Slaa aliyemwita rafiki na msiri wake.

“Sio jambo la kujivunia kupoteza askari mmoja ukiwa vitani, lakini hatuwezi kurudi nyuma, tunachopigania ni zaidi ya Dk. Slaa, Mbowe na Lowassa. Wakati wa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 1995, Dk. Slaa alikuwa CCM, alikuwa mwana CCM mpaka mwezi mmoja na nusu kabla ya uchaguzi akaja Chadema tukiamini kuwa ni mtu mwema na mkweli.

“Alikuwa mwema na kweli tukaendelea na safari pamoja, mwanzo sikuomba kuwa mwenyekiti wa Chadema lakini niliombwa na wazee nikakataa wakanilazimisha nikawaambia nitakubali uenyekiti kama chama kitaruhusu Dk. Slaa awe Katibu Mkuu,” alisema Mbowe.

Alisema baada ya sharti hilo na Dk. Slaa akawa Katibu Mkuu wa chama na wakaanza kile alichokiita safari ya kujenga chama.

Alisema baada ya kumaliza miaka mitano akaombwa tena kuongoza chama kabla ya mwaka 2000 kusimamisha mgombea urais kwa mara ya kwanza.

“Nasema haya ili kila mmoja akiondoka hapa aondoke akijua historia, mwaka 2000 nikaombwa tena kugombea nikatoa tena sharti la kuwa na Dk. Slaa kuwa Katibu Mkuu, ilipofika 2010 nikapendekeza agombee urais, akaniambia sihitaji madaraka nikamwambia nenda Watanzania watakusaidia.

“Dk. Slaa akawa mgombea, nafasi ya urais unapewa na wenzio baada ya kuwekwa kwenye kipimo. Mwaka huo huo katika mazingira anayoyajua Mungu, ndugu yangu, rafiki yangu kwa mapenzi yake alianza mahusiano yake ya kifamilia, akawa sio yule anayemjua Mbowe, ilivyofika 2014 akasema mwenyekiti naomba safari hii uwe mgombea.

“Nikasema hapana, Dk. Slaa bado una nafasi, kwa hiyo tumekaa vikao vya chama nikapeleka pendekezo kwamba mgombea awe yeye, Kamati Kuu ya chama wakaniambia mwenyekiti kwanini unaleta pendekezo, nikasema ndani ya Chadema hatuwezi kugombania uongozi kwa sababu wapo waliokufa na walioachika kwa sababu ya chama, kuna gharama kubwa tumetumia kujenga chama hiki na hiyo siyo ya Mbowe ni ya Watanzania wote.

“Nitakuwa mtu wa mwisho kuona chama hiki kinapasuka kwa sababu ya mtu yeyote, nikaiambia Kamati Kuu ni lazima tunavyotoka na jina la mgombea tuwe salama, tukitoka na jina tusiwe na aibu ya kulitekeleza,” alisema Mbowe.

Alisema Chadema kinajengwa kisayansi na si kwa ushabiki hivyo kiliamua kufanya utafiti kwa gharama kubwa kwa kuzitumia kampuni kutoka Marekani na Afrika Kusini pamoja na mshauri kutoka Uingereza ambao hawakuwa wakimjue yeye Mbowe, Dk. Slaa wala Lowassa.

Alisema walichotakiwa kufanya watafiti hao ni pamoja na kuangalia uwezo wa Chadema kushika uongozi wa Serikali katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 ikiwa na Dk. Slaa, kujua mambo ya msingi ambayo Watanzania wanafikiri ni kipaumbele kwa Serikali ijayo na tatu ni mgombea gani wa CCM atakayeisumbua Chadema kwenye kuleta mabadiliko.

Mbowe alisema jambo jingine walilopaswa kufanya wachunguzi hao ni kuangalia kinachopaswa kufanyika ili kufanikisha kwa usalama uchaguzi mkuu.

“Majibu hayakuwa mazuri na Dk. Slaa anajua, wakatuambia Chadema mna nguvu lakini hamuwezi kuwa na nguvu mkiacha CCM salama, wakasema tufanye juu chini, tukeshe tukiomba CCM isiingie uchaguzi mkuu ikiwa imara. Pasueni CCM, katika utafiti ule, hata Lowassa sijamwambia, katika utafiti ule tuliambiwa atakayetusumbua akiwa CCM ni mtu mmoja tu, ni Lowassa, wakatuambia mkiwa na mgombea wenu, Dk. Slaa na Lowassa akawa CCM ana watu CCM na ndani ya Chadema watamuunga mkono. Siku hiyo tulikaa na Dk. Slaa tukiangaliana kwa dakika 10 hakuna wa kuongea,” alisema Mbowe.

Alisema baadaye Dk. Slaa alimfuata na kumwambia iwapo Lowassa atakatwa na CCM wamchukue ama la na yeye alimjibu kwa kumuuliza ikiwa hivyo anataka nafasi gani na kwamba alichagua kuendelea na nafasi yake ya Katibu Mkuu hivyo alimwachia mengine akaendelea nayo, lakini aliporudi nyumbani balaa likaanzia hapo.

“Dk. Slaa akiona wakati wowote bado kuna nafasi na akijisikia kuja tumpokee, kama ataona watu wote ambao ni kinywa cha Mungu ila yeye na mkewe ndio wako sawa tumsamehe tuende mbele, tuliamua tumkamate Lowassa na tayari ameisaidia Chadema.

“Kwa sababu ya Lowassa sasa hivi tunaye Waziri Mkuu wa zamani, Frederick Sumaye na Mwanasiasa mkongwe, Kingunge Ngombale Mwiru. Naomba hoja ya Dk. Slaa tuiweke pembeni kwa kuwa mabadiliko ya nchi yetu ni muhimu kuliko Slaa na Mbowe,” alisema.

Kwa upande wake, Mzee Kingunge alisema ingawa alisomeshwa na Tanu na kuitumikia lakini ameamua kuhama CCM iliyozaliwa na Tanu kwa sababu imebinafsishwa.

“Siwezi kuendelea kuwa huko kwa sababu siwezi kukubali watu ambao hawaheshimu katiba yao wenyewe na wana CCM ambao ni wanachama wa dhati, wajifikirie wenyewe mmoja mmoja na kuamua,” alisema Kingunge.

Naye Lowassa aliposimama kuzungumza na wananchi wa Karatu, alisema umati wa watu uliojitokeza kumsikiliza unashabihiana na uliokuwa Arusha juzi na aliwaomba wananchi hao kumpa kura ili aweze kushinda na hatimaye abadilishe maisha yao kwa kuanza na elimu anayoamini ni msingi wa kila kitu.

Wakati huo huo mwandishi, Safina Sarwatt anaripoti kutoka Moshi kuwa, shughuli za uzalishaji na usafiri mjini Moshi jana  zilisimama kwa muda baada ya wafuasi na wanachama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kujitokeza kwa maelfu barabarani wakishangilia ujio wa mgombea urais kupitia chama hicho, Edward Lowassa.

Wananchi hao walianza kujitokeza barabarani saa 1:30 asubuhi wakiwa na mabango na bendera ya vyama vinavyoundwa na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), wakizunguka katika mitaa mbalimbali ya mji wa Moshi na kusababisha shughuli za uzalishaji uchumi kusimama.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles