23.3 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Lissu, Mbowe mbaroni

Mwandishi Wetu, Dar es salaam

JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam limesema linawashikilia baadhi ya viongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kwa tuhuma za kuratibu maandamano.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa alieleza kuwa licha ya viongozi hao kusema kuwa maandamano hayo ni ya amani, lakini wamebaini uwepo wa vitendo vya uvunjifu wa amani na uharibufu wa mali za wananchi.

Aliwataja viongozi wanaoshikiliwa na jeshi hilo kuwa ni Freeman Mbowe, Godbless Lema na Boniface Jacob.

“Kama ilivyotokea Oktoba 29 na 30 nilitoa taarifa kwa umma kwamba tumesikia fununu kuwa kuna watu ambao wamesema hawakubalini na matokeo ya uchaguzi na kwamba wanapanga kuingia mitaani kufanya vurugu kama sehemu ya kuonesha kuwa hawakubaliani na maamuzi ya wananchi.

“Tulitoa katazo kwamba kitendo hicho hakikubaliki. Suala la kuingia kwenye ushindani wa kutafuta ridhaa ua kuchaguzliwa lilianza kwa kuuza sera, ni masuala sasa ya kuacha mikononi mwa wananchi wenyenyewe ndio waamue kiongozi gani anayewafaa.

“Na tumepiga marufuku maandamano hayo lakini wote walioshindwa mikoani huko sasa wanajikusanya Dar es Salaam na wanachokifanya sasa ni kutangaza kuratibu na kusimamia maandamano ambayo tuliyakataza, kwamba yangefanyika kuanzia asubuhi ya jana.

“Na walichokifanya wamekuwa wakifanya vikao mbalimbali ambavyo kwa kupitia watu wetu wa taarifa fiche wamekuwa wakiendelea kuwapa taarifa za namna wanavyoendeela kupanga na kuratibu maandamano hayo, lakini kibaya zaidi ni kwamba maandamano hayo yaliambatana na maelekezo yaliyotolewa kwa watu walioshawishika kwamba pamoja na kuandamana, wangeendelea kufanya uharibifu wa miundombinu, walipanga kuchoma masoko, lakini pia walipanga kuchoma vituo vya mafuta na walipanga kuchoma magari ambayo wangekutana nayo wananchi wakienda kazini au wakitoka kazini kwenda majumbani,” alisema.

Alisem akutokana na mpango huo walitarajia kufanya fujo kubwa ambayo walikuwa wameipanga, ambapo wamekusanya viongozi mbalimbali kutoka katika maeneo yote wakiwemo akina Joseph Mbilinyi (Sugu), Lema na wengine ambao wamekuja kwa ajili ya kufanya oparesheni hizo.

Alisema wameshawakamata baadhi ya wengine na kwa sasa oparesheni kubwa inaendelea na yeyote anayeshiriki kuratibu, kuendesha au kuingi barabarani atakutana na mkono wa sheria.

“Nilisema hilo tayari Mbowe, Lema na Jacob tumeshawakamata, tunao na kijana ambaye ni tunda la kushawishiwa tayari tunaye hapa na oparesheni inaendelea, wote wanaohusika watakanatwa na wanaendelea kuhojiwa na mwisho ni kukamilisha utaratibu wa kuandaa jalada kwa ajili ya kwenda mahakamani,” alisema Kamanda Mambosasa.

“Tunawashikilia viongozi hao kwa kuwa wanashawishi vijana kuandamana ili kutekeleza vitendo vya kiuhalifu, na kinara mmoja aitwaye Issack Lulandala amekamatwa akiwa  anahamasisha vijana kuandamana.

“Baada ya mahojiano alikiri kupewa kazi hiyo na viongozi wa Chadema, ikiwa sambamba na kuhatarisha usalama wa raia na mali zao. Leo walipanga kuwatumia vijana kuchoma moto miundombinu na masoko,” alisema Mambosasa.

Alisema usiku wa kuamkia jana polisi walifanya msako kuwakamata wanaodaiwa kuwashawishi  vijana kushiriki maandamano, kuharibu mali kama kuchoma magari, kuchoma visima vya mafuta, kuchoma matairi ili kuvuruga amani na kuleta taharuki ili shughuli za wananchi zisimame.

Alidai wanaoshawishiwa ni vijana ambao hawana woga na wavuta bangi na waathirika wa dawa za kulevya.

Baada ya Rais John Magufuli kutangazwa kuwa rais kwa awamu ya pili siku ya Ijumaa usiku, baada ya Uchaguzi Mkuu uliofanyika  Oktoba 28, viongozi wa vyama vikuu vya upinzani nchini Tanzania walitangaza kutokubaliana na matokeo hayo na kuitisha maandamano leo hii.

Vyama vikuu vya upinzani nchini Tanzania Chadema na ACT-Wazalendo vinataka kurejewa kwa Uchaguzi Mkuu huo.

Vyama hivyo viwili vinapinga matokeo ya uchaguzi wa Jumatano ambapo rais aliye madarakani, John Magufuli amekwishatangazwa mshindi.

Katika mkutano wa wanahabari wa pamoja baina ya viongozi wa Chadema na ACT Wazalendo vyama hivyo pia viliitisha maandamano yasiyo na ukomo ya nchi nzima ili kudai kurejewa kwa uchaguzi huo.

Mwenyekitiwa Chadema Taifa, Freeman Mbowe alieleza kuwa: “kilochofanyika si uchaguzi ni unyang’anyi wa demokrasia uliofanywa na ZEC (Tume ya Uchaguzi Zanzibar) na NEC (Tume ya Taifa ya Uchaguzi) .

Vyama hivyo sasa vinataka kuvunjwa kwa Tume ya NEC na ZEC.

Vyama hivyo aidha viliwaomba Watanzania kufanya maandamano ya amani.

“Kuanzia Jumatatu (jana), wanachama wa vyama vyetu na wote wasiokubaliana kushiriki katika maandamano ya amani kuanzia Novemba 2 hadi hapo madai yetu yakapotelekezwa,” walisema.

Siku ya Alhamisi Mwenyekiti wa ACT Wazalendo ambaye pia alikuwa mgombea wa urais visiwani Zanzibar, Maalim Seif Seif Sharif Hamad alikamatwa pamoja na viongozi wengine wa chama hicho.

Kamanda wa Polisi Mjini Magharibi Zanzibar Awadhi Juma alisema Maalim Seif alikamatwa akiwa anafanya maandamano ambayo hayana kibali akiwa na wafuasi wa chama chake.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles