25.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Ligi Kuu Bara yasimamishwa

Winfrida Mtoi, Dar es Salaam

WAKATI mataifa mbalimbali duniani yakihaha kudhibiti virusi hatari vya corona, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imetangaza kusimamisha shughuli za michezo yote nchini, ikiwamo Ligi Kuu Tanzania Bara, Ligi Daraja la Kwanza, Ligi Daraja la Pili.

Uamuzi huo umekuja siku mbili, baada ya Wizara ya Tawala la Mikoa na Serikali za Mitaa(Tamisemi) kupitia waziri wake Suleiman Jafo, kupiga marufuku Umoya wa Michezo na Taaluma ya Shule za Msingi(Umitashumta)  na Umoja wa Michezo ya Shule za Sekondari(Umiseta).

Zuio hilo la serikali litadumu kwa siku 30.

Juzi Waziri wa Afya, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu alitangaza kugundulia kwa mgonjwa wa kwanza hapa nchini aliyepatikana mkoani Arusha mwenye maambulizi ya virusi vya corona.

Akizungumza jijini Dar es Salaam jana kupitia Televisheni ya Taifa(TBC), Waziri Mkuu,  Kassim Majaliwa, serikali imefikia uamuzi huo wa kusimamisha shughuli zote zenye mikusanyiko ili kuzuia kuenea kwa ugonjwa huo hapa nchini.

“Serikali inasimamisha mikusanyiko yote  mikubwa ya ndani na nje ikiwamo matamasha ya muziki na michezo yote, pamoja na ile ya mashirika ya uma inayofanyika kila mwaka,” alisema Majaliwa.

Waziri Mkuu aliitaka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kuyaandikia barua mashirikisho yote juu ya uamuzi huo wa serikali.

Muda mfupi baada ya agizo la Waziri Mkuu, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), lilitoa taarifa ya kutekeleza kwa kuvunja kambi ya timu ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars.

Stars ilikuwa kambini ikijiandaa na mchezo wa kusaka nafasi  ya kufuzu fainali za mataifa ya Afrika(Afcon) dhidi ya Tunisia na michuano ya Afrika kwa wachezaji wanaochezaji ligi za ndani(Chan).

Hata hivyo, Shirikisho la Soka Afrika(Caf), limesitisha michezo yote ya kusaka tiketi ya Afcon pamoja na michuano ya Chan, ambayo ilitarajiwa kuanza Aprili 4 hadi 25 nchini Cameroon.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo iliyotolewa na Ofisa Habari wa TFF, Clifford Ndimbo, Kamati ya Uongozi ya Bodi Ligi Kuu ambayo inatarajia kukutana leo itatoa muelekeo wa utekelezaji wa agizo hilo.

“Wanachama na wadau wetu wote, watekeleze agizo la serikali na kusitisha shughuli za michezo yote katika ngazi zote,” ilisema taarifa ya Ndimbo.

Baadhi ya ligi maarufu duniani zilizosimamishwa kutokana na tishio la corona ni  Ligi Kuu ya England maarufu EPL, Ligi Kuu Italia inayofahamika zaidi Serie A  na Ligi Kuu Hispania, La Liga.

Ugonjwa wa corona ulianzia nchini China kabla ya kusambaa maeneo mengine duniani, huku ukisababisha vifo vya maelfu ya watu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles