24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

LEODEGER TENGA AFUNGUKA MIPANGO MIZITO BMT

Na THERESIA GASPER-DAR ES SALAAM


MWENYEKITI wa Baraza la 14 la Michezo la Taifa (BMT), Leodegar  Tenga, ametaja malengo matano ambayo chombo hicho kimepanga kuyatekeleza katika kipindi cha miaka mitatu ijayo.

Akizungumza Dar es Salaam na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Tenga alisema  michezo ina faida kubwa  kwa jamii kwa kuwa inatoa ajira,  hujenga afya na kutumika katika mambo mbalimbali yanayohusu ulinzi na usalama pamoja na utunzanji wa mazingira, hivyo lazima ipewe kipaumbele.

Rais huyo wa zamani wa TFF, aliyataja malengo hayo kuwa ni kufanya tathmini ya hali halisi ya maendeleo ya michezo nchini na kutumia tathmini hiyo kutengeneza mpango mkakati wa kitaifa wa maendeleo ya michezo nchini unaolenga kuliwezesha Taifa kuondokana na upungufu uliopo hivi sasa.

Alisema BMT itafanya mapitio ya sera ya michezo na sheria iliyoundwa chombo hicho ili iendane na hali halisi pamoja na matakwa ya maendeleo ya michezo ya wakati huu na  kufanya mikutano yenye tija na wadau wa michezo katika ngazi za taifa, mkoa na wilaya.

Tenga alisema wataendelea kutoa mafunzo ya utawala bora na namna nzuri ya kuongoza vyama na mashirika ya michezo ili kupunguza changamoto mbalimbali, ikiwemo migogoro isiyo ya lazima na kuleta ustawi katika kuendeleza michezo nchini.

Pia alisema watahakikisha vyama vya michezo vinaheshimu katiba zao kwa kuheshimu vipindi vya uongozi na kufanya uchaguzi muda unapofika, ikiwa ni pamoja na kutoa taarifa ya utendaji, mapato na matumizi yao.

“Katika hili itasaidia kupunguza migogoro isiyo ya lazima, pia viongozi wa michezo lazima wazingatie utawala bora, wawajibike na wawe wazi katika utendaji wao,” alisema Tenga.

Mikakati iliyowekwa

Alisema ili kufikia malengo hayo, Baraza hilo lina mikakati  iliyojiwekea ambayo ni  kukusanya maoni ya wadua wa michezo yao ili kubaini changamoto zinazoikabili sekta ya michezo nchini.

Alisema watashirikiana na wadau wengine kutoa mafunzo kwa vyama na mashirikisho ya michezo kuhusu uandaaji wa mpango mkakati, uandaaji wa maandiko ya biashara pamoja na dhana ya utawala bora.

“Katika hili tutapokea maoni yatakayounda baraza pamoja na tathmini ya hali ya michezo nchini, pia hii itasaidia kuvijengea uwezo vyama katika kujiendesha na kusimamia klabu zilizo chini yao.

“Tutahakiki uhai wa vyama na mashirikisho yote yaliyosajiliwa kitaifa kwa kuangalia utendaji wake wa majukumu, ikiwemo uendeshaji wa vikao vya kikatiba, kutimiza matakwa ya uchaguzi na programu za uendeshaji wa michezo husika.

“Tutaitisha vikao kazi vya kamati za michezo za mikoa, vyama vya mashirikisho ya michezo, wadhamini na wadau wengine kujadili namna bora ya kuendeleza sekta ya michezo, ikiwa ni pamoja na kuibua vipaji na kuviendeleza kuanzia katika ngazi za shule ya msingi na kuendeleza miundombinu ya michezo.

“Tutahamisha ujenzi wa miundombinu na upatikanaji wa vifaa vya michezo nchini, tutavihamasisha vyama na mashirika ya michezo kushiriki na kuchangia katika shughuli za kuelimisha jamii kama vile kusaidia katika kampeni za kitaifa za chanjo kwa watoto, kupambana na Ukimwi, kutokomeza malaria na kupiga vita dawa za kulevya,” alisema Tenga na kuongeza:

“Wanamichezo hatuna budi kutimiza wajibu huu wa kuendeleza jamii kwa kuwa michezo haiwezi kuendelea bila ya kuwa na jamii yenye afya bora na inayoendelea, pia viongozi na wanamichezo lazima tuwe mabalozi wa kampeni za kitaifa zinazolenga kuilinda na kuiendeleza jamii yetu.

“Kujijengea uwezo katika mapato kwa kusimamia vyanzo vya mapato vilivyopo na  kubaini vyanzo vipya ili kuliwezesha baraza kutekeleza majukumu yake kikamilifu.”

Tenga alitoa wito kwa vyama na mashirikisho ya michezo nchini kumiliki ofisi, kutengeneza mipango ya maendeleo ya michezo husika na kuwa na bajeti itakayoainisha mapato na matumizi.

“Lazima hesabu za vyama na mashirikisho zikaguliwe na nakala halisi za taarifa za ukaguzi huo ziwasilishwe kwa msajili wa vyama na klabu za michezo Tanzania kama sheria inavyoelekeza.

“Ni jambo la kushangaza na haieleweki hata kidogo kwa vyama na klabu za michezo kutokuwa na anuani za makazi zinazoonyesha maeneo ya ofisi zao au kutokuwa na akaunti za benki, kwani kimsingi vyama na mashirikisho ya taifa ya michezo ni vyombo vya watu wengi vinavyoongozwa kwa mujibu wa katiba zao zenye kuzingatia sheria za nchi,” alisema Tenga.

Alisema pamoja na kusajiliwa kama vyama na mashirikisho ya watu binafsi, vinatarajiwa viendeshwe kwa kufuata maadili yanayosimamia utendaji wa vyombo vya umma.

“Nizikumbushe klabu, vyama na mashirikisho ya michezo kuzingatia kanuni za Baraza la Michezo la Taifa za mwaka 199, kifungu cha 7 kinachozungumzia utaratibu wa kukata rufaa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles