28.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

LATRA yasitisha leseni za usafirishaji abiria kwa mabasi 22

Na Beatrice Kaiza, Mtanzania Digital

MAMLAKA ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) imesitisha leseni za usafirishaji abiria kwa mabasi 22 kwa kipindi cha mwezi Januari hadi Februari, 2023.

Akizungumza na waandishi wa habari Februari 21, 2023 jijini Dar es Salaam Mkurugenzi Udhibiti Usafiri wa Barabara LATRA, Johansen Kahatano amesema Hatua hii ni kutokana na vitendo vya kuingilia Mfumo wa Kufuatilia Mwenendo wa Magari (VTS) na kusababisha mfumo kutotuma taarifa ama kutuma taarifa kwa kurukaruka (skipping).

Aidha amesema Mamlaka imewaandikia barua watoa huduma ambao vifaa vya kufuatilia mwenendo wa magari yao (VTDs) vinaonyesha viasharia vya kuchezewa na kuwataka watoe maelezo ya kwanini leseni zao zisisitishwe kutokana na kasoro hizo.

“Hapa kuna baadhi ya mabasi ambayo baada ya wataalamu wa Mamlaka kufanya uchunguzi, waligundua betri za vifaa vya kufuatilia mwenendo wa mabasi (VTDs) zimeharibiwa na mfumo wa umeme kubadilishwa.

“Uchunguzi wa magari hayo bado unaendelea na pale itakapothibitika kuwa kuna uvunjaji wa kanuni leseni za magari husika zitasitishwa,” amesema Kahatano.

Amesema kitendo cha kuingilia Mfumo wa VTS ni ukiukwaji wa Kanuni ya 51 ya Kanuni za Leseni za Usafirishaji (Magari ya Abiria) za Mwaka 2020, hivyo, Mamlaka imechukua hatua ya kusitisha leseni hizo kwa mujibu wa Sheria ya LATRA ya Mwaka 2019 na Kanuni zake za mwaka 2020.

“Kabla ya kurejeshewa leseni zao, watoa huduma wa mabasi husika walitakiwa kuwafikisha Jeshi la Polisi madereva wa mabasi husika ili wachukuliwe hatua kwa mujibu wa Sheria ya Usalama Barabarani Sura ya 168.

“Mamlaka inawatahadharisha wamiliki wa mabasi na madereva wao kuzingatia Kanuni za Leseni za Usafirishaji (mabasi ya abiria) za Mwaka 2020 na Sheria ya Usalama Barabarani Sura ya 168 kwa kuongeza usimamizi wa huduma,” amesema Kahatano.

Katika hatua nyingine Kahatano amesema Jumla ya madereva 13,291 wameshasajiliwa kwenye mfumo Wao na kati yao madereva 904 wameshafanya mitihani kwa ajili ya kuthibitishwa

hivyo aliwaagiza wamiliki wote wa magari yanayotoa huduma kibiashara kuhakikisha madereva wao wote wamesajiliwa ifikapo Aprili 30, 2023.

“Usajili unafanyika kwenye ofisi zote za LATRA Tanzania Bara na hivyo madereva wote waelekezwe kufika kwenye ofisi za LATRA ili waweze kusajiliwa,” amesema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles