30.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

KUWA MAKINI NA VITU HIVI KATIKA MALEZI

 

 

NA AZIZA MASOUD,

WAZAZI ni nguzo kubwa katika malezi ya mtoto, matokeo ya tabia za mtoto yanatokana na malezi mazuri aliyopewa na mzazi.

 Malezi anayoyapata mtoto kuanzia umri wa siku moja mpaka miaka 13 ndiyo yanayochangia kumtengeneza mtoto.

Kama mzazi kuna vitu vya msingi unapaswa kuwa mwangalifu lakini kati ya hivyo vipo  vinne vya muhimu zaidi.

Kitu cha kwanza kuwa makini sana na adhabu unazompa mtoto, hatua za kinidhamu unazochukua dhidi ya mtoto wako zinaweza kumjenga ama kuathiri malezi yake. 

Si lazima kila kosa umwadhibu unaweza kufanya malezi shirikishi pia, kila unapomkataza mtoto kufanya jambo fulani kama vile kutoa lugha chafu kwa watu, utoro shuleni, ugomvi n.k toa  sababu za kufanya hivyo.

Ni vizuri zaidi ukawa unamfahamisha ni kwanini haifai kufanya jambo fulani, ili kumpatia nafasi ya kuhoji/kutafakari/kuelewa badala ya kumshurutisha tu kutekeleza maagizo. 
Kwa kufanya hivyo, unampa uwezo wa kupambanua, kuelewa na kujiamini katika maamuzi mbalimbali.

 Hatua kali za kinidhamu kama vile kumchapa mtoto zinaweza kumsababishia hofu ambayo huathiri uwezo wao wa kuwasiliana na wewe, walimu hata wenzao pia. 

Hata hivyo, pia haitakiwi kuwa mpole mno kwa sababu watoto wanaweza kuendelea kuwa wakosefu wa nidhamu na kuathiri mwenendo wao katika jamii na shuleni.

Mazingira ambayo yanajumuisha hali ya hewa, watu wanaokuzunguka, vitu vilivyopo pia yanaweza kuchangia kuathiri malezi ya mtoto.

Mazingira humfanya mtoto kuwa tofauti, mfano anayetoka kwenye nyumba ambayo wazazi wake wako katika hali ya ugomvi kila mara, umasikini, utajiri n.k. lazima watakuwa tofauti.

Wazazi tuna wajibu wa kuwawekea mazingira mazuri watoto ili waweze kukua katika maadili mema.

Jambo jingine ni mawasiliano, wazazi mnapaswa kuwashirikisha watoto katika mawasiliano na baadhi ya maamuzi ya kifamilia endapo atahitajika.

Hiyo itamfanya kuwa na uhuru wa maamuzi kumuuliza mtoto leo unataka kula nini mama/baba ni kuonyesha kuthamini mawazo yake. 

Pia katika maongezi, nina maana mtoto akisema jambo lolote ni muhimu kumsikiliza na si vizuri kumpuuza au kumkaripia kwamba anapiga kelele.

 Tabia hiyo itamsaidia kwa kumpatia uwezo wa kujieleza na kujisikia kuthaminiwa na wazazi wake. 

Mfumo wa malezi pia  unaweza kumjenga mtoto wako au kumharibu. 

Weka ratiba ya kukaa na watoto na kuongea nao na kusikiliza mawazo hayo kuwajengea hali ya kujisikia kuthaminiwa na kupendwa na wazazi/walezi na hivyo  kuwaongezea furaha na amani. 

Pia tabia hii huwajengea hali ya kujiamini na uhuru wa kueleza hisia zao nyumbani na shuleni bila hofu kwa sababu ya imani ya kupendwa imejengwa kwenye akili zao.
 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles