24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

KOREA KASKAZINI YATANGAZA MKAKATI WA KUISHAMBULIA MAREKANI

PYONGYANG, KOREA KASKAZINI

KOREA Kaskazini jana ilitangaza mpango wake wa kurusha kombora kuelekea kisiwa cha Guam, kituo kikuu cha kijeshi cha Marekani kilichopo Bahari ya Pasifiki, ambako imeweka ndege zake za kivita.

Televisheni ya Taifa ya Korea Kaskazini ilimwonyesha Mkuu wa Mikakati Jeshini, Kamanda Kim Rak Gyom, akisoma tamko linalochambua undani wa namna kombora hilo litakavyorushwa.

“Makombora ya Hwasong-12 yatakayorushwa na Jeshi la Watu wa Korea yatavuka anga la Shimane, Hiroshima na Koichi nchini Japan kwa umbali wa kilomita 3,356.7 kwa sekunde 1,065 kabla ya kutua baharini umbali kati ya kilomita 30 hadi 40 kutoka kisiwa cha Guam,” inasema taarifa hiyo.

Kwa mujibu wa Kamanda Gyom, maroketi hayo yanapangwa kurushwa kabla ya mwishoni mwa wiki ijayo.

Kisiwa hicho kidogo kina wanajeshi 7,000 wa Marekani kwenye vituo vyake viwili, na kinakaliwa na wakazi 160,000.

Ni jambo la nadra sana kwa Korea Kaskazini kutangaza undani wa urushaji wake wa makombora kama hivi ilivyofanya jana, lakini endapo kweli itachukua hatua hiyo, hicho kitakuwa kitendo kikubwa cha uchokozi kuwahi kufanywa na nchi hiyo ndani ya kipindi chote cha mzozo wake na Marekani.

Tamko hili la sasa linaashiria kilele cha mzozo wa maneno baina ya Pyongyang na Washington, baada ya juzi Rais Donald Trump wa Marekani kuionya Korea Kaskazini kuwa ingekabiliana na ‘moto na ghadhabu’ ikiitisha Marekani.

“Kiongozi wa Korea Kaskazini amekuwa akitishia, na kama nilivyosema, Korea Kaskazini itakumbana na moto, ghadhabu na nguvu za kweli, ambazo kamwe hazijawahi kushuhudiwa duniani hapo kabla,” Trump alionya.

Shirika la Habari la Serikali ya Korea Kaskazini (KCNA), limeileleza kauli hiyo ya Trump kuwa ni kitisho kilichojaa upuuzi, na kwamba jeshi la nchi hiyo linapanga kuvishambulia vikosi vya adui kwenye vituo vyake kisiwani Guam na kutuma onyo muhimu kwa Marekani.

Kwa upande mwengine, Korea Kusini imeitolea wito Korea Kaskazini kuacha kufanya mambo ambayo yataleta maafa kwenye Rasi ya Korea.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles