29.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

KOCHA SIMBA AWATOA WASIWASI MASHABIKI

NA THERESIA GASPER –DAR ES SALAAM


Ligi Kuu Tanzania Bara inatarajia kuendelea leo kwa mechi nne huku Simba wakiwa wageni dhidi ya JKT Tanzania kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Tanga.

Mechi nyingine zitakuwa kati ya Alliance ambao watawakaribisha Singida United katika Uwanja wa CCM Kirumba Mwanza, huku Mtibwa Sugar wakiwa wenyeji dhidi ya Ruvu Shooting dimba la Manungu, Morogoro na Biashara United dhidi ya Mbao FC katika dimba la Karume, Musoma.

Kwa takribani misimu miwili Simba hawajacheza katika Uwanja wa Mkwakwani baada ya timu za Tanga kushuka daraja msimu wa mwaka 2016.

Wekundu hao wa Msimbazi watashuka dimbani huku wakijiamini kutokana na ushindi mnono walioupata wa mabao 5-0 dhidi ya Ruvu Shooting kwenye Uwanja wa Taifa Dar es Salaam mwishoni mwa wiki iliyopita.

Timu hiyo inayonolewa na kocha mkuu, Patrick Aussems, imekuwa ikipata matokeo mazuri kutokana na ubora wa kikosi hicho msimu huu.

Ikumbukwe kuwa mara ya mwisho timu hizo kukutana ilikuwa msimu wa mwaka 2016/17 kabla ya timu hiyo ya JKT Tanzania kushuka daraja.

Katika mechi ya raundi ya kwanza ya msimu huo timu hizo zilipokutana kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam walitoka suluhu ya kutofungana na waliporudiana mzunguko wa pili Simba ilipata ushindi wa bao 1-0 katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Upande wao JKT Tanzania wanashika nafasi ya tano katika msimamo wa ligi wakijikusanyia pointi 18 wakiwa sawa na Mbeya City pamoja na Mbao FC wakitofautiana kwa idadi ya mabao ya kufunga na kufungwa.

Kikosi cha JKT Tanzania kinachonolewa na kocha mkuu, Bakari Shime, kitakutana na Simba kikiwa na kumbukumbu ya kuibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Tanzania Prisons katika Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo uliopo Mbweni Dar es Salaam.

Kocha mkuu wa Simba, Aussem, alisema kwa rekodi nzuri walizokuwa nazo katika mechi za hivi karibuni, wataingia uwanjani wakiwa na morali ya juu ili kuendeleza ushindi kwa mara nyingine.

“Nafahamu mechi za ugenini zinakuwa na ushindani mkubwa ukizingatia na uwanja unakuwa si mzuri, hivyo lazima tuwe makini ili tupate pointi tatu muhimu,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles