27.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 18, 2024

Contact us: [email protected]

KMC Yaifundisha soka Yanga

 ZAINAB IDD I-DAR ES SALAAM 

TIMU ya KMC imeibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Yanga, katika mchezo wa kirafiki uliochezwa jana Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam. 

Timu hizo zinajifua kujiweka sawa kwa mwendelezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, ambayo imepangwa kuanza Juni 13. 

Yanga imepangwa kuendeleza kampeni zake za Ligi Kuu msimu huu ambao unaelekea ukingoni, kwa kuumana na Mwadui FC ya mkoani Shinyanga, wakati KMC itapepetana na timu inayomilikiwa na Jeshi la Kujenga Taifa(JKT), Ruvu Shooting. 

Hivi karibuni,Serikali iliruhusu shughuli za michezo kuendelea, baada ya maambukizi ya ugonjwa wa corona kupungua kwa kiasi kikubwa hapa nchini. 

Ikumbukwe kwamba, Machi 17 mwaka huu, Serikali ilipiga marufuku shughuli zinazosababisha mikusanyiko, ikiwemo michezo, baada ya ugonjwa wa corona kuthibitishwa kuingia nchini. 

Ugonjwa huo ambao kwa mara ya kwanza uligundulika nchini China, umesababisha vifo vya maelfu ya watu duniani. 

Katika mchezo wa jana, KMC inayomilikiwa na Manispaa ya Kinondoni ilienda mapumziko ikiwa mbele kwa mabao 2-0, yaliyofungwa dakika ya 31 na Sadallah Lipangile na Charles Ilanfya dakika ya 45. 

Kwa ujumla kipindi cha kwanza, KMC ilionekana kutawala mchezo na kutengeneza nafasi nyingi za kufunga huku wachezaji wake wakionekana wepesi, hali iliyowapa fursa ya kupata mabao hayo. 

Kipindi cha pili, KMC iliingia uwanjani na mkakati wa kusaka mabao zaidi huku 

 Yanga ikiwa na lengo la kusawazisha.

Hata hivyo, maji yalionekana kuzidi unga kwa upande wa Yanga kwani ilijikuta ikichapwa bao la tatu na KMC lililofungwa dakika ya 65 kwa mkwaju wa adhabu na kiungo mshambuliaji Hassan Kabunda.

Dakika tisini za mchezo huo zilikamilika kwa KMC kutakata kwa ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Yanga.

Siku moja kabla ya mchezo huo, Kocha Msaidizi wa Yanga, Charles Mkwasa, aliweka wazi kuwa anatarajia watakutana na hali ngumu ya kusaka matokeo mazuri dhidi ya KMC, akitaja sababu kuwa ni baadhi ya wachezaji wake kuonekana kuongezeka uzito.

Alisema anatarajia wapinzani wao watakuwa bora zaidi yao kwakua walianza kujifua mapema zaidi yao.

Mchezo huo ulihudhuriwa na mashabiki wengi, pengine ni kutokana na kiu waliyokuwa nayo kwa muda mrefu baada ya kuikosa burudani ya soka kutokana na janga la ugonjwa wa corona.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles