LONDON, ENGLAND
KOCHA wa Liverpool, Jurgen Klopp, amesisitiza kuwa amemwomba msamaha kocha wa Everton, Marco Silva, kwa kitendo chake cha kuingia uwanjani akishangilia baada ya bao la ushindi la dakika za lala salama lililofungwa na Divock Origi.
Kocha Silva alikataa kupokea ombi hilo la msamaha lakini uamuzi huo haukumfanya Klopp kushindwa kushangilia ushindi huo.
Klopp, aliingia uwanjani akishangilia kwa kumkumbatia kipa wake, Alisson Becker, baada ya bao hilo lililofungwa dakika ya 90.
Hata hivyo, kitendo hicho cha Klopp kinaweza kumgharimu na kuitwa na Chama cha Soka England (FA), ili kutoa maelezo.
Klopp alisema: “Baada ya mchezo nilimwomba msamaha kocha Silva. Nilimweleza kiasi gani ninaheshimu kazi yake akiwa kocha wa timu hiyo. Everton ni washindani wa kweli.
“Mchezo wa watani wa jadi ni mgumu kweli, lakini huu ulikuwa tofauti katika miaka michache iliyopita. Basi ni kitu gani naweza kusema? Sikutaka kukimbia ndani ya uwanja, haikuwa mipango yangu, wala sikuhitaji kukimbilia kwa Becker, lakini hali hii hutokea.
“Kwa yote yaliyotokea dakika 95 tena kwa heshima zangu zote kwa Everton ni timu nzuri. Timu zote zilikuwa vizuri katika kupambana, ulikuwa mchezo mzuri wa watani wa jadi.
“Ubora wetu ulikuwa katika kupiga pasi fupi pamoja na kushambulia kwa kushtukiza. Tulijaribu kuumiliki mchezo lakini ilikuwa vigumu kwetu kufanya hivyo.”
Kocha Silva alisema Klopp hakuwa ameomba msamaha: “Hakuomba msamaha kwangu. Niwe mkweli sikuona wala kusikia akisema neno samahani kwangu. Sidhani kama alitarajia kitu kama kile kingetokea. Ilikuwa bahati yao kushinda lakini huu ni mchezo wa mpira.