25.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Kituo cha Utalii nyuki kuanzishwa uyui

Na Allan Vicent, Tabora

Chuo Cha Mafunzo ya Ufugaji Nyuki (BTI) kilichoko mkoani Tabora kinatarajia kuanzisha kituo cha Utalii wa nyuki (Apitourism) kupitia mradi wake wa mafunzo ya ufugaji nyuki uliopo katika kijiji cha Mayombo kata ya Magiri wilayani Uyui.

Hayo yamebainishwa Julai 20, 2021 na Mkuu wa Chuo hicho, Semu Daudi katika taarifa yake kwa Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Luteni Josephine Mwambashi ambapo alimweleza kuwa mafunzo hayo endelevu yanafanyika katika Msitu wa Hifadhi Simbo uliopo katika kijiji hicho.

Amesema mkakati wao ni kuboresha msitu huo kwa kujenga mazingira mazuri ya kiuhifadhi ili pawe eneo maalumu la kiutalii ambapo shughuli mbalimbali ikiwemo mafunzo ya ufugaji nyuki kwa vitendo yatakuwa yakitolewa.

Alibainisha kuwa BTI ni chuo pekee hapa nchini kinachotoa elimu ya ufugaji nyuki kwa vitendo katika ngazi ya Astashahada na Stashahada na kwa sasa kina wanafunzi 408 kutoka mikoa mbalimbali hapa nchini na nchi jirani ya Kenya.

Alisema chuo kilikabidhiwa msitu huo na Wakala wa Huduma za Misitu (TFS) ili kuutumia kuendeshea mafunzo ya ufugaji nyuki kwa vitendo kwa wanafunzi wake na jamii kwa ujumla.

Semu amebainisha manufaa ya mradi huo kuwa ni kuendesha shughuli za mafunzo  kwa wafuga nyuki, jamii kupewa mbinu bora za ufugaji nyuki na uhifadhi mazingira na kupata fursa ya kufanya kwa vitendo shughuli hizo.

Alitaja manufaa mengine kuwa ni kuongeza uzalishaji wa mazao yatokanayo na nyuki (asali na nta), kutoka wastani wa tani 550 kwa mwaka kwa sasa, hivyo kuongeza kipato kwa wananchi na serikali kwa ijimla.

Aidha alieleza kuwa jamii inayoishi jirani na eneo hilo wataruhusiwa kuvuna mazao mengine yasiyo ya mti (non wood forest) kama vile dawa, uyoga na mbogamboga.

Alifafanua kuwa mradi huo umegharimu kiasi cha sh mil 58.2 ambazo zilitumika kutengeneza mizinga 500, ujenzi wa banda la kufugia nyuki (bee cage) na kuweka mipaka ya kudumu (beacons), na kuongeza kuwa gharama hizo zilichangiwa na Chuo (mil 57) na TFS sh mil 1.2.

Mkuu huyo alisisitiza kuwa wataendelea kuboresha mazingira ya msitu huo ili kuongeza thamani yake ambapo watatenga eneo mahsusi kwa ajili ya ufugaji nyuki wa kisasa kwa wanajamii, eneo la utafiti, mafunzo, na eneo la utalii wa nyuki.

‘Tunatarajia kuanzisha kituo cha utalii wa nyuki (Apitourism) katika msitu huu, hili ni eneo maalumu ambapo shughuli za utalii wa nyuki zitakuwa zikioneshwa kwa watu mbalimbali’, alisema.

Aidha aliongeza kuwa ili kulifanya eneo hilo lenye ukubwa wa hekta 324.6 kuwa kituo kikubwa cha uzalishaji mazao ya nyuki, wanatarajia kuongeza idadi ya mizinga kutoka 500 ya sasa hadi kufika 800.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles