NA WINFRIDA MTOI, DAR ES SALAAM
KIUNGO wa timu ya Azam, Salum Abubakar ‘Sure Boy’, ameamua kufanya mazoezi ya mchezo wa masumbwi, wakati huu ambao Ligi Kuu Tanzania Bara imesimama.
Serikali imepiga marufuku kwa siku 30, shughuli zinazosababisha mikusanyiko ya watu ikiwemo michezo, ikiwa ni tahadhari ya kuepuka kusambaa ka virusi vinavyosababisha ugonjwa wa corona ambao tangu uliporipuka nchini China na kisha kusambaa mataifa mengi umesababisha vifo vya maelfu ya watu.
Ni kutokana na marufuku hiyo ya Serikali ambayo ilianza Machi 17, Ligi Kuu Tanzania Bara, Ligi Daraja la Kwanza na Ligi Daraja la Pili na mashindano mengine yanayosimamishwa na Shirikisho la Soka Tanzania(TFF) yalisimamishwa.
Hatua hiyo ilizifanya klabu kuwapa mapumziko wachezaji wao, huku zikisubiri tamko jingine la Serikali kuruhusu kuendelea kwa shughuli michezo pale hali itakapokuwa shwari.
Nyota wengi wa soka duniani, wamekuwa wakitupia video zikionyesha wanavyotumia mapumziko yao wakiwa majumbani, baadhi wakionekana kupiga danadana, lakini kwa Sure Boy, yeye ameamua kuja kwa staili tofauti.
Katika video iiyotupiwa jana katika mtandao wa Klabu ya Azam, Sure Boy, anaonekana akiwa na mtu anayemfanyisha mazoezi na masumbwi.
Video hiyo iliambatana na maneno ya lugha ya kingereza yanayosemaa: “Stay At Home Challenge”.