24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

KIONGOZI WA UPINZANI ASHITAKIWA KWA UHAINI KENYA

NAIROBI, KENYA


MMOJA wa viongozi wa upinzani nchini Kenya, Miguna Miguna ameshtakiwa kwa kosa la uhaini.

Miguna alihusika katika kuapishwa kwa kiongozi wa upinzani, Raila Odinga.

Miguna alishtakiwa kwa kuhudhuria na kuidhinisha kiapo alichokula Raila, kushiriki katika mkutano ulio kinyume cha sheria na kuhusika na masuala ya kihalifu.

Alifikishwa mbele ya Mahakama ya Kaunti ya Kajiado, maili 50 Kusini mwa Nairobi, ambako ndiko wafuasi wa upinzani walidhani amefichwa.

Hayo yalielezwa jana na Mwendesha Mashitaka Mkuu Msaidizi, Nicholas Mutuku katika Mahakama Kuu mjini Nairobi ikiwa ni siku kadhaa tangu Miguna akamatwe na kushikiliwa mahali pa siri licha ya Mahakama kuamuru aachiwe kwa dhamana ya Sh 50,000 za Kenya, Ijumaa iliyopita.

“Kwa mara nyingine serikali inakiuka haki za Miguna kwa kumsafirisha kutoka eneo moja hadi lingine bila ya kuijulisha familia au wakili mawakili wake,” ilisema timu yake ya sheria.

Wakati huo huo, Seneta James Orengo pamoja na wabunge wengine 10 watakaa bila wasiwasi wa kukamatwa na maafisa wa polisi kwa kushiriki katika hafla ya kumwapisha Odinga, siku saba zilizopita.

Jaji Luka Kimaru, amekwishatoa agizo kwa polisi kutowasumbua wala kuwakamata wanasiasa hao pamoja na bilionea, Jimmy Wanjigi.

Hata hivyo, Jaji Kimaru amewaagiza wajisalimishe kwa Mkurugenzi wa Idara ya Uchunguzi wa Makosa ya Jinai (DCI), Geoffrey Kinoti kesho saa tano mchana ili wahojiwe.

Wakati hayo yakijiri, mahakama pia imetoa amri wabunge 141 wa Nasa warudishiwe walinzi na bastola zao zilizokuwa zimechukuliwa na serikali.

Jaji Roselyn Aburili ameagiza bodi ya kikosi cha polisi inayoidhinisha watakaopewa silaha iwarudishie silaha walizokuwa wamepokonywa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles