23.3 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Kinara wa teleza Kigoma akamatwa

Na Editha Karlo

-Kigoma

VYOMBO vya dola mkoani hapa vimefanikiwa kumkamata Hussein Hamis, anayetuhumiwa kuwa kinara wa ubakaji na kujeruhi wanawake nyakati za usiku maarufu kama teleza.

Hamis aliye maarufu kwa jina la Orosho, alikamatwa pamoja na watuhumiwa wengine tisa wakitambuliwa kama teleza, ambao huwaingilia kingono wanawake kwa kuwalazimisha, kuwaibia na kuwajeruhi wakiwa wamejipaka ‘oil’ chafu au mafuta ya mawese ili wanaposhikwa wawe wanateleza.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, Mkuu wa Wilaya ya Kigoma Mjini, Samson Hanga alisema baada ya kuwapo taarifa hiyo, vyombo vya dola viliendesha  msako mkali kwa kushirikiana na wananchi ili kuwakamata wahalifu.

“Tulitengeneza namna bora ya kuwakamata wahusika, tulifanya kazi ya upigaji kura ya siri tukapata majina, mengine tulipata kupitia vyombo vya dola. Mpaka sasa tumekamata vijana tisa, wapo mahabusu na upelelezi unaendelea,” alisema Hanga.

Alisema katika majina yaliyotajwa na kupigiwa kura, mtuhumiwa mmoja alitajwa na akina mama waliofanyiwa vitendo vya ukatili ambaye ni Hamis.

“Unajua Serikali ina mkono mrefu, macho makubwa, yule kijana alipopata taarifa tunamtafuta alikimbilia kwa mama yake Kijiji cha Kagongo, baadae akakimbilia tena Kijiji cha Kagunga, juzi jioni tukafanikiwa kumkamata wilayani Kasulu na kuletwa hapa kituo cha polisi kwa ajili ya hatua zaidi,” alisema.

Hanga alisema pia wamefanya gwaride la utambuzi kwa waathirika  kuwatambua vijana 10 waliokamatwa.

Alisema msako bado unaendelea na kuonya yeyote anayejihusisha na vitendo hivyo kuacha mara moja kabla vyombo vya dola havijambaini na hatua kali zitachukuliwa dhidi ya wale wote watakaobainika.

Mmoja wa waathirika wa matukio hayo, Hadija Khamis mkazi wa Mwanga Kusini, Manispaa ya Kigoma Ujiji, aliishukuru Serikali kwa kufanikiwa kuwakamata vijana hao.

“Unajua hadi sasa yaani siamini kama kweli teleza amekamatwa, tulikuwa tunaishi bila ya amani, mimi alipoingia kwangu alinikata na panga mara nne, hapa nina maumivu makali hata kazi siwezi kufanya,” alisema.

Mkurugenzi wa Asasi ya Women Promotion Center, Martha Jerome alisema suala la teleza linaumiza mioyo, hivyo wanaiomba Serikali kusaidiana na jamii kulitokomeza.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles