31.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

KIFO CHA MWANAFUNZI NIT KILIVYOWAGUSA MASTAA BONGO

NA CHRISTOPHER MSEKENA

SIMANZI zimetawala kila kona ya nchi kufuatia kifo cha mwanafunzi wa mwaka wa kwanza katika Chuo Cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Akwilina Akwilini aliyeuwawa kwa risasi  Ijumaa wiki iliyopita wakati polisi wakiwatawanya wafuasi wa CHADEMA waliokuwa wakiandamana eneo la Mkwajuni, Kinondoni, Dar es salaam.

Gumzo la kifo hicho cha kusikitisha kilichomkuta Akwilina aliyekuwa ndani ya Daladala akielekea Bagamoyo kupeleka barua za mafunzo kwa vitendo, limekuwa kubwa kiasi cha kusababisha salamu za pole zikimiminike kwa ndugu, jamaa na marafiki kutoka kila pande ya nchi.

Mastaa ndani ya kiwanda cha burudani wameguswa pia na kifo hicho. Kwa njia mbalimbali wametoa salamu za pole na mitazamo yao baada ya kuumizwa na Akwilina aliyezikwa jana nyumbani kwao mkoani Kilimanjaro.

Swaggaz linakusogezea jumbe mbalimbali za pole na maoni ya mastaa  wa muziki na filamu Bongo kama ifuatavyo.

Billnas

Staa huyu ambaye alihudhulia shughuli za kuagwa kwa mwili wa Akwilina kwenye viwanja vya chuo cha NIT, Mabibo Dar es salaam alikutana na Swaggaz na kusema: ‘Sisi kama wasanii tunapaswa kushiriki kwenye matatizo ya kijamii kama haya, ndiyo maana nimekuja hapa kumuaga Akwilina, pole nyingi ziende kwa familia maana nafahamu walivyoumia,” anasema Billnas.

Jokate Mwegelo

Alitumia ukurasa wake wa Instagram kusema: “Aquilina Akwilini Baftaha, umefariki ukiwa kijana mdogo sana, kwa wakati ambao ndiyo haswa unatakiwa katika jamii. Kifo chako kimetushtua na kimetugusa,

“Haswa kwa namna ambayo umepoteza maisha kama mshumaa uliozimwa ghafla. Hukustahili kufa kwa namna ulivyouawa,
Mwenyezi Mungu awape nguvu, imani na amani ndugu na jamaa wako wa karibu,” anasema Jokate.

Lady Jay Dee

Naye alisema: “Hakuna mzazi yoyote angependa kumpoteza mtoto wake katika umri huu tena kwa kifo cha namna hii, Mwenyezi Mungu atuondolee roho za kikatili na kuwaongezea huruma wenye mamlaka na silaha duniani,” anasema.

Vanessa Mdee

Alionyeshwa kuguswa na kifo kwa kusema: “Huwa sizungumzii siasa ila siku zote nazungumzia masuala ya vijana haswa watoto wa kike, pole zangu kwa ndugu jamaa na marafiki wa Akwilina, Mungu awape wepesi,” anasema.

Jacquline Wolper

Anasema: “Aisee! nimeumia sana kwa sababu nilisikia jana (siku ya tukio ) bunduki zikipigwa nikiwa ofisini kwangu kila mtu anakimbia yaani ilinijia picha ya Iraq na siyo Tanzania ile niliyoizoea, kila mtu anafunga biashara zake na wengine wanaacha biashara zao wanakimbia daaa imeniuma sana baada ya kujua pia kuna mwanafunzi kafariki,”.

Diamond Platnumz

Mkali huyo wa Bongo Fleva alitumia ukurasa wake wa Instagram kusema: “Mwenyezi Mungu aipe nguvu familia ya marehemu na kuilaza roho yake mahala pema peponi, Amin,”.

Mwana FA

Anasema: “Maisha na ndoto za binti asiye na hatia yamekatishwa. Najua hatuna uwezo wa kumrudishia uhai na ndoto zake lakini ni matumaini yangu hata tutaona uwajibikaji wa wahusika, Taifa halina watu wenye mioyo ya kujipima, kuna kiumbe kamtoa binti roho na watu wapo wapo tu huoni hata kama wanajiuliza kweli walikosea au kama wamekosea kabisa. Ajabu kabisa,” .

Shilole

Anasema: “Tumbo la uzazi limeniuma jamani R.I.P katoto kazuri kasikokuwa na hatia,”.

Joh Makini

Anasema:Ukivaa viatu vya uhusika tofauti tofauti wa tukio hili ni maumivu makali, Mungu atuepushie kazi ya shetani juu ya watu wake tusielekee kule, R.I.P Akwilina,” anasema.

ROMA

Anasema: ‘ Akwilina umekufa kipindi cha mwezi wa toba tena Ijumaa ya kwanza ya njia ya msalaba, damu iliyomwagika msalabani ni agano kwetu, risasi moja imegharimu ndoto nyingi.

“Nnawaza pengine ulikuwa na ndoto za kuja kiongozi wa Taifa hili, ndoto zimezima kama mshumaa, pengine wazazi wamewekeza kukusomesha ili uje uwasaidie, nani atawasaidia, pengine risasi ile ingeweza kumpata mtoto wangu au mtoto wako wewe. Pengine zinaweza kuwa nyingi ila ukweli, Akwilina umetuliza wengi,” anasema Roma.

 

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles