25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Kiama wasioendeleza mashamba yao

Na RAMADHAN HASSAN – DODOMA

WAZIRI wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi, amesema wafanyabiashara wakubwa na baadhi ya wabunge, wameitumia ardhi kama mtaji wa kukopea huku mashamba yakiwa hayaendelezwi.

Kutokana na hali hiyo amesema kati ya mashamba makubwa 2,000, Serikali imechukua 46 kutokana na wahusika kushindwa kuyaendeleza. Alisema hayo akihitimisha mjadala wa taarifa ya utekelezaji wa shughuli za Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Januari 2018 hadi Januari 2019.

Waziri Lukuvi alisema watu wengi wakiwemo wabunge na wafanyabaishara wamekopea mashamba makubwa pamoja na kuwekea rehani ili mambo yao yaweze kwenda vizuri.

“Lakini wako watu wengi sana ambao wamekopea mashamba haya, matokeo yake siku zote hizi za nyuma walikuwa wanayatumia kwa ajili ya kuweka rehani kupata mtaji wa kufanya biashara nyingine.

“Hapa mbele yangu nimekuja na daftari hili, mimi nina ‘privilege’ ya kujua siri zenu ninyi wote, humu ndani kuna watu ambao wamepewa ardhi na wamechukua mkopo, hapa kuna zaidi ya Sh trilioni moja nimeshika.

“Hapa kuna fedha taslimu zaidi ya Sh bilioni 800 watu wamekopa kwa kuweka rehani ya ardhi, lakini ninyi wenyewe mnajua hivi kama kweli kilimo cha Tanzania kingewekezwa zaidi ya Sh trilioni moja, si lazima nchi  ingetikisika?

“Jiulizeni fedha ziko wapi, sasa sisi tunao ushahidi baada ya kufanya uhakiki kwamba watu walichukua hizi fedha kwa sababu usimamizi ulikuwa hafifu, wamechukua kama kinga, wamechukua benki pamoja na kuandika madhumuni ya kuendeleza yale mashamba, lakini benki hazifuatilii.

“Benki zinataka tu ‘return’ ya biashara zao, watu wameenda kuwekeza Dubai, wamenunua ‘apartment’, wamewekeza biashara za kulipa papo kwa papo, mashamba yamebaki mapori na hayakuendelezwa.

“Sasa hivi wabunge mkisema kuna mashamba pori huku watu wamekopa hela benki, lakini watu wanapambana kulima yale mashamba halafu anatokea mtu siku moja anatishatisha, miaka 10, 20 yeye anaendelea kuongeza thamani ya kampuni yake kutokana na mtaji unaotokana na thamani ya ardhi,” alisema.

Aliwahakikishia wabunge atasimamia ilani ya CCM ya kufanya uhakiki na kuyachukua mashamba hayo. Aliitaja mikoa ambayo Serikali imechukua mashamba kuwa ni Arusha mawili, Kilimanjaro moja, Dar es Salaam mawili, Morogoro 18, huku Kilosa peke yakiwa ni 12, Iringa moja, Pwani manne, Simiyu mawili, Tanga 17, Kagera moja, Mara moja na Lindi moja.

“Kwa hiyo kutokana na maelekezo yenu tumefuatilia, tumerudisha yale maeneo kwa maelekezo yenu na katika uhakiki  wa yale mashamba 2,000 mpaka sasa ni miaka mitatu hii tumeshafuta mashamba 46 kwa mujibu wa sheria, lakini chanzo ni ninyi.

“Katika hawa watu 2,000 tuliowapa hati wanayo mashamba makubwa, hati hizi ukipewa kuna masharti ya matumizi huku nyuma, umri wa matumizi umeandikwa kwenye hati hizi.

Hati hizi hakuna umri wa matumizi, lakini unatakiwa ukipata hilo shamba angalau uhangaike walao 1/8 kwa mwaka uliendeleze,” alisema Lukuvi.

AMJIBU MSIGWA Mbunge wa Iringa Mjini, Peter Msigwa (Chadema) akichangia taarifa hiyo, alisema baadhi ya wafanyabiashara na viongozi wastaafu wameonewa kwa kunyang’anywa mashamba. Akijibu Lukuvi alisema; “hakuna sababu ya kuunda kamati teule, kamati teule ya kwenda kuchunguza kazi aliyoifanya Rais, kisheria ninyi mnaofikiria maneno haya hangaikeni na majimbo yenu tu.”

MASHAMBA YA MOHAMED ENTERPRISES

Kuhusu mashamba ya Kampuni ya Mohamed Enterprises, alisema anamiliki 21 katika maeneo ya Tukuyu, Rungwe, Mombo, Korogwe na Same.

“Na yote hayo sasa asipoendeleza tunafanyaje? Kwanza niwaambie mashamba yaliyofutwa ni sita, lakini onyo alipata mashamba 12, baada ya kupata onyo, ofisa ardhi pale akawa anachezacheza Naibu Waziri akamdhibiti, amemwondoa.

“Lakini baada ya hapo nilivyomwagiza Naibu Waziri tumepiga na picha na vielelezo vyote tunavyo, tukagundua ukweli, mashamba sita …

Kwa habari zaidi jipatie nakala yako ya gazeti la MTANZANIA.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles