27.5 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Kenyatta amtumia Lowassa kuwapasha Watanzania

RAIS wa Kenya, Uhuru Kenyatta.
RAIS wa Kenya, Uhuru Kenyatta.

Na Mwandishi wetu, Kenya

RAIS wa Kenya, Uhuru Kenyatta, amemtumia Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, kufikisha salamu kwa Watanzania kwa kuwaeleza kwamba amekalia kiti cha moto, lakini anakimudu na ataendelea kukikalia.

Lowassa ambaye pia ni mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, tangu juzi yupo nchini Kenya kwenye mazishi ya Waziri wa zamani wa Serikali ya nchi hiyo, William Ole Ntimama aliyefariki dunia Septemba 2, mwaka huu na kuzikwa jana.

Ntimama aliyefariki dunia nyumbani kwake katika Kaunti ya Narok, anatajwa kama kiongozi aliyejitolea kuhudumia taifa lake, na hasa jamii ya Wamaasai, kwa kupinga dhuluma za kihistoria pamoja na msimamo wake wa kuutetea Msitu wa Mau.

Akizungumza kwenye msiba huo, Rais Kenyatta alisema kuwa licha ya changamoto zilipo nchini humo, hasa kuelekea Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika mwakani, hana wasiwasi na kiti chake.

“Ninamuona hapa jirani na ndugu Mheshimiwa Lowassa (Edward), ambaye amekuja hapa pia na ujumbe wake kutoka Tanzania, ninataka nikuhakikishie kwamba kiti ni moto, lakini ukirudi Tanzania waambie nimekikalia sawa sawa kabisa, hakuna shida.

“Raila (Odinga) ndugu yangu, leo (jana) hakuna mambo ya Jubilee kwani haina mikono miwili, sisi tupo na mkono mmoja tunajua mahali tunaelekea, nyinyi rekebisheni nyumba yenu tukutane kwenye uwanja, achana na nyumba yangu ya Jubilee,” alisema Kenyatta.

Pamoja na hali hiyo, alisema hakuna shida lakini akaonya kama kutafuta nafasi ya urais kufanyike polepole kwani yeye amekalia kiti na hana haraka ya kuondoka.

“Hakuna shida tutafute  hii kitu (urais) polepole, nyinyi mnatafuta sisi tumekalia kiti na hatuna haraka ya kuondoka, niliambiwa hapa nikiwa pake, kuna mswahili mmoja alitajwa hapa kwamba watu waelezwe kumeza mate sio kula nyama, kwa hiyo wenzetu endeleeni,” alisema Kenyatta huku akishangiliwa.

Raila ambaye ni hasimu mkubwa wa Rais Kenyatta, amekuwa na urafiki wa karibu na Rais Dk. John Magufuli.

LOWASSA ALONGA

Akizungumza juzi na mwandishi wa BBC nchini Kenya, John Nene, Lowassa alisema kuwa alitarajia kwamba Rais Magufuli angeondoa urasimu serikalini, lakini bado kuna mambo ndani ya Serikali yake hayajakwenda sawa. Hata hivyo alipobanwa afafanue aligoma kufanya hivyo.

Kauli hiyo ya Lowassa imekuja huku Serikali ikiendelea na marufuku ya kuzuia mikutano ya hadhara pamoja na ile ya ndani kwa vyama vya siasa.

Aprili 2, mwaka huu Waziri Mkuu wa zamani wa Kenya, Raila Odinga, alimtembelea Rais Magufuli aliyekuwa kwenye mapumziko kijijini kwake Kilimani, Wilaya ya Chato mkoani Geita.

Akizungumza baada ya kuwasili Chato, Raila alisema yeye na familia yake wapo likizo na wamekuja kumtembelea rafiki wa familia yao kwa lengo la kumsalimia.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles