33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Katibu wa CCM Mwanza apongeza uhamasishaji wa Sensa

Na Clara Matimo, Mwanza

Katibu wa Chama Cha Mapinduzi(CCM), Mkoa wa Mwanza, Julius Peter ameipongeza Serikali kwa kuweka mipango mizuri na kuwahamasisha wanachi kushiriki katika zoezi la sensa ya watu na makazi ambalo limeanza Agosti 23, 2022 nchi nzima.

Amesema kwa siku ya kwanza ya zoezi hilo ameridhishwa na mwitikio wa wananchi kwa jinsi wanavyotoa ushirikiano kwa makarani wa sensa  hiyo ni kutokana na hamasa waliyoipata kutoka serikalini hivyo wametambua umuhimu wa zoezi hilo kwa mustakabali wa maendeleo yao na taifa kwa ujumla.

Peter ametoa pongezi hizo Agosti 23, 2022 alipozungumza na Mtanzania Digital muda mfupi baada ya kuhesabiwa na karani wa sensa ya watu na makazi mwaka 2022, Theodatha Theonest katika makazi yake yaliyopo Mtaa wa Nyakabungo B Kata ya Isamilo Wilaya ya Nyamagana Mkoa wa Mwanza.

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Adam Malima akizungumza na Karani wa sensa ya watu na makazi 2022, katika  Mtaa wa Isamilo Kaskazini B Dotto Selemba, alipokuwa akihesabiwa katika makazi yake  Kata ya Isamilo Mtaa wa Isamilo Kaskazini B Wilaya ya Nyamagana.

Amesema tangu asubuhi zoezi la sensa lilipoanza linaenda vizuri wananchi wa mkoa huo wanahamasa kubwa sana kuhusiana nalo hali hiyo inaashiria kwamba litafanyika kwa ufanisi mkubwa ambapo ametoa rai kwa wananchi ambao hawajafikiwa na makarani wa sensa waendelee kuwa wavumilivu na watulivu lakini pia watakapofikiwa watoe ushirikianoa kwa kujibu maswali watakayoulizwa kwa usahihi.

“Naishukuru sana serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kweli imefanya kazi nzuri sana ya hamasa kwa wananchi kuhusu zoezi la sensa ambalo linaendelea nchini kote hasa katika mkoa wetu  wa Mwanza,”amesema Pater na kuongeza:

“Najua makarani wanajituma naamini kwa siku saba ambazo wametengewa kwa ajili ya kufanya zoezi hili watalifanya kwa ufasaha maana leo tu tumeshuhudia jinsi wanavyojituma nawasihi waendelee na kasi hii hii waliyoanza nayo leo ili tupate takwimu sahihi ambazo zitakisaidia Chama cha Mapinduzi  kutekeleza ahadi ilizozitoa kwa wananchi mwaka 2020 kiliponadi ilani yake kilisema kitasogeza huduma za kijamii karibu zaidi na wananchi,” amesema.

Lengo la sensa hii ni kujua  idadi ya Watanzania,  huduma wanazozihitaji na jinsi ya kuwafikishia huduma hizo maana lazima uwe na takwimu ili upange mipango yako kikamilifu hivyo zoezi hili la sensa linaloendelea litatupa takwimu sahihi za watu walioko katika mkoa wa Mwanza, Wilaya na Tanzania kwa ujumla ili tunaposema tunaleta maendeleo mfano huduma za afya tunajua tunawahudumia watu wangapi katika huduma hiyo,”amesema Katibu huyo.

Kwa upande wake Karani wa sensa ya watu na makazi 2022, katika Mtaa wa Nyakabungo B, Theodatha Theonest amesema tangu alipoanza zoezi hilo asubuhi hajapata changamoto yoyote huku akibainisha kwamba watu wote aliowafikia katika makazi yao amewakuta wakiwa majumbani mwao wanasubiri kuhesabiwa na wamempa ushirikiano.

“Ombi langu watu ambao hawajafikiwa wazidi kuwa na subira tutawafikia hakuna mtu ambaye ataachwa katika kaya yake bila kuhesabiwa wote watahesabiwa ndani ya siku zilizopangwa kwa ajili ya sensa binafsi naahidi kufanya kazi kwa ufanisi.

“Lakini kama kuna watu ambao hawatoi ushirikiano kwa makarani wenzangu wa sensa nawasihi sana watoe ushirikiano kwa kutoa taarifa zao sahihi wasikilize wito wa serikali kwa sababu taarifa hizo ndiyo mipango ya maendeleo kwa miaka 10 ijayo, wakitoa taarifa zitaisaidia serikali kupanga bajeti kwa ajili ya mahitaji mengine mengi ya kijamii wasifikili kwamba sensa ni kwa ajili ya mambo mengine tofauti na maendeleo wajue ni kwa ajili ya faida yao wajiandae kuhesabiwa ili kuweza kufanikisha malengo ya taifa letu,”amesema Theodatha.

Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Nyakabungo B, Kata ya Isamilo mkoani Mwanza, Martini Mathiasi amesema “Mimi kwenye eneo langi toka tulipoanza zoezi la sensa leo asubuhi hadi sasa saa kumi na moja jioni hatujapata changamoto yoyote, mwitikio wa watu ambao wamehojiwa na makarani wa sensa ni mzuri hiyo imetokana na kuanza mapema kuwahamasisha na kuwaelimisha wananchi kuhusu umuhimu wa zoezi hili.

“Rai yangu kwa wananchi ambao hawajafikiwa na makarani wa sensa walipende zoezi hili maana ni la kitaifa lakini pia linafaida kwao kwa sababu takwimu zitakazopatikana zitatumiwa na serikali kuwaletea maendeleo  kwa hiyo  niwaombe waendelee kutoa ushirikiano kwa makarani na wale ambao wamebanana na shughuli zao waache taarifa sahihi majumbani  lakini wanaemuachia taarifa wawe na uhakika kwamba ni mtu ambaye anaweza akatoa taarifa zao vizuri,”amesisitiza Mathias.

Aidha, katika mkoa wa Mwanza viongozi mbalimbali wamehesabiwa akiwemo Mkuu wa Mkoa huo, Adam Malima aliyehesabiwa na karani wa sensa ya watu na makazi, 2022, Dotto Selemba katika makazi yake  Kata ya Isamilo Mtaa wa Isamilo Kaskazini B Wilaya ya Nyamagana ambaye pia alitoa rai kwa wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwa makarani wa sensa ili zoezi hilo lifanyike kwa ufanisi mkoani humo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles