27.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

KAMPUNI 136 ZAJITOKEZA KUWEKEZA VIWANDA  

Na PETER FABIAN-MWANZA


mtz9MKURUGENZI Mtendaji Mkuu wa Kituo cha Uwekezaji Nchini (TIC), Clifford Tandari, amesema tangu Rais Dk. John Magufuli aingie madarakani Novemba 2015 hadi sasa, kampuni 136 zimejitokeza kuwekeza viwanda nchini.

Akizungumza juzi na waandishi wa habari jijini Mwanza, Tandari alisema hatua hiyo ni utekelezaji wa azma ya Serikali ya awamu ya tano kuifanya Tanzania kuwa ya viwanda kwa kuhakikisha vinajengwa viwanda vikubwa, vya kati na vidogo katika maeneo mbalimbali nchini.

“Kituo cha TIC kimeishafikiwa na wawekezaji wa kampuni 136 za ndani na mataifa ya nje yanayotaka kuwekeza kwa kujenga viwanda vikubwa, vya kati na vidogo hapa nchini, nasi TIC tumewahakikishia kuwa tutahakikisha vikwazo na changamoto, ikiwamo upatikanaji wa maeneo ya uwekezaji havitakuwa kikwazo,” alisema.

Tandari alitoa wito kwa kampuni mbalimbali zinazokusudia kuwekeza kufika TIC ili kupata ushauri na kuwasaidia kukamilisha taratibu za kisheria za kuwekeza ili wanapopata matatizo waweze kusaidiwa kwa kuwa wanakuwa na mikataba ya kitaifa na kimataifa ya sheria ya uwekezaji.

Naye Meneja wa TIC Kanda ya Ziwa, Fanuel Lukwalo, alizitaja baadhi ya kampuni zilizojitokeza kuwekeza ni Nyanza Bottiling Ltd (Mwanza) inayotaka kupanua kiwanda kuongeza uzalishaji wa vinywaji baridi, Mwanza Hollidring Ltd inayotaka kujenga kiwanda cha saruji Busega mkoani Simiyu.

Nyingine ni Premidis Ltd iliyo mbioni kujenga kiwanda cha vinywaji vya vileo wilayani Nyamagana, MRS Wang ya China inayotaka kujenga kiwanda cha kukausha mabondo ya samaki wilayani Ilemela na CMG Ltd ya jijini Mwanza inayojenga kiwanda cha kutengeneza nguzo za umeme za saruji.

Katika hatua nyingine, Tandari alisema baadhi ya wafanyabiashara kutoka ndani na nje ya nchi, wanaotaka kujenga viwanda, wamedai kuwa na hofu juu ya upatikanaji wa umeme na maji ya uhakika kwa saa zote jambo linaloweza kuwaingiza katika hasara.

Alisema baadhi ya wawekezaji ambao wanafanya mchakato wa kuwekeza kwa kujenga viwanda katika mikoa ya Mwanza na Simiyu, wamekuwa wakikumbana na changamoto hizo.

Tandari alisema kwamba tayari Serikali imezipokea changamoto hizo na imeanza kuzitafutia ufumbuzi wa haraka ili kampuni hizo zisiache kuwekeza viwanda katika maeneo mbalimbali nchini.

Aidha alisema TIC itashirikiana na wizara, taasisi na mamlaka nyingine za Serikali kuhakikisha suala la ucheleweshaji wa leseni unamalizika haraka na kampuni zote zinajenga viwanda haraka kama ilivyokusudiwa na Serikali.

“TIC tumejipanga kushughulikia changamoto mbalimbali na kuzitafutia ufumbuzi wa haraka zinazofikisha kwetu na wawekezaji wa ndani na nje ya nchi ili kuondoa urasimu na ucheleweshaji unaoweza kuwakwamisha wawekezaji wa viwanda, hoteli na utoaji huduma nyingine za kijamii,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles