23.9 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Kamati ya Siasa ya CCM Pwani yapata sura mpya

Na Gustafu Haule, Pwani

Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Pwani wamemchagua, Mansoor Musa Said na wenzake wawili kuwa wajumbe wa Kamati ya Siasa ya mkoa huo.

Mansoor amechaguliwa katika uchaguzi uliofanyika Februari 14, mwaka huu katika ukumbi wa ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani iliyopo Kibaha Mjini ambapo mbali na Mansoor wengine waliochaguliwa ni Hussein Kasama na Dk. Chokawa Tindwa.

Katika uchaguzi huo Mansoor aliibuka mshindi kwa kupata kura 55 wakati Dk. Tindwa akishinda kwa kura 62 huku Hussein Kasama akipata kura 38 kati ya 75 zilizopigwa.

Akitangaza matokeo ya uchaguzi huo Katibu wa CCM Mkoa wa Pwani, Hassan Mwinyi, amesema kuwa katika uchaguzi huo kulikuwa na wagombea tisa lakini washindi ni watatu ambao kura zao ni nyingi kuliko za wagombea wengine.

Amesema kuwa, kamati ya siasa ya Mkoa wa Pwani ilikuwa na pengo la wajumbe watatu na sasa imekamilika baada ya kupata wajumbe wapya ambao wamechaguliwa Februari 14.

“Katika uchaguzi wetu tulikuwa na wagombea tisa na wajumbe halali 75 lakini walioshinda ni wale waliopata kura nyingi kuliko wenzao hivyo nawatangaza washindi wetu kuwa ni Mansoor Musa Said, Dk.Tindwa na Hussein Kasama,”amesema Mwinyi.

Aidha, Mwinyi amewataja wagombea wengine walioingia katika kinyang’anyiro hicho kuwa ni Hussein Chuma (14), Catherine Shayo(13), Said Nassoro(6), Hussein Gama(5) na Hamisi Kitogole(9).

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kutangazwa kuwa mshindi Mansoor amewashukuru wajumbe kwa kumchagua na kwamba kilichobaki ni kukitumikia Chama.

Amesema kamati ya siasa ni chombo kikubwa cha maamuzi katika mkoa husika na kwamba kazi yake ni kutenda haki huku akisema anakwenda kumtendea haki kila mmoja kwa mujibu wa kanuni za chama.

“Nawashukuru wajumbe mara mbili,kwanza walinichagua kuwa mjumbe wa Halmashauri kuu ya Mkoa na leo wamenichagua tena kuwa mjumbe wa kamati ya siasa hivyo nami nitakwenda kufanyakazi kikamilifu kwa kufuata misingi ya haki,” amesema Mansoor.

Mansoor amesema kuwa kwasasa uchaguzi umekwisha na amewaomba wagombea wenzake kuvunja makundi ili wafanyekazi moja ya kujenga chama kwani kushinda au kushindwa yote ni matokeo ya CCM.

Nae Dk. Tindwa, amewashukuru wajumbe kwa kumpa kura nyingi zilizopelekea kushinda katika nafasi hiyo huku akiahidi kufanyakazi kikamilifu ili kuhakikisha Chama kinaimarika zaidi na hatimaye kuendelea kushika dola katika chaguzi zijazo.

Dk. Tindwa ,amewasisitiza wana CCM pamoja na wagombea katika uchaguzi huo kuacha makundi kwakuwa nafasi iliyobaki ni kushirikiana katika kuhakikisha ilani ya Chama inatekelezwa kwa kiasi kikubwa ili ifikapo 2024 na 2025 wapate la kuwaambia wananchi.

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Pwani, Mwishehe Mlao amesema kuwa wajumbe wa kamati ya siasa waliochaguliwa wapewe ushirikiano katika kutekeleza majukumu yao bila kuletewa nongwa.

Mlao amesema kuwa wapo baadhi ya wabunge wanadhani mjumbe wa kamati  ya siasa akipita katika maeneo yao labda anataka jimbo lake jambo  ambalo sio sahihi.

Amesema  kuwa,kipindi hiki ni kipindi ambacho wajumbe hao wanapaswa kufanyakazi zao kwa ajili ya kukijenga chama na kwamba masuala ya  uchaguzi ni mwaka 2025  na kwa mujibu wa kanuni kila mwanachama anapaswa kuchukua fomu bila kikwazo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles