23 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Kafulila aagiza waliotafuna fedha za makusanyo ya Halmashauri wasakwe

Na Derick Milton, Simiyu

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, David Kafulila ameagiza kusakwa na kuwekwa ndani watu wote ambao wanadaiwa kuhusika katika upotevu wa kiasi cha Sh milioni 38 za makusanyo ya ushuru kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Busega.

Kafulila ametaka kila mtu ambaye amehusika kwenye upotevu wa fedha hizo, akamatwe kisha awekwe ndani na atatoka mara baada ya kurejesha kiasi ambacho anadaiwa na halmashauri.

Uamuzi wa Mkuu huyo wa mkoa umekua kufuatia ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa halmashauri hiyo, kuonyesha kuna kiasi cha Sh milioni 38 zilikusanywa kupitia mashine za kukusanya ushuru za elektroniki (POS) lakini hazikupelekwa benki.

Kafulila amesema kitendo cha watu hao kushindwa kuwasilisha pesa hizo ambazo walikusanya kupitia mashine hizo ni kitendo cha wizi, hivyo lazima hatua kali zichukuliwe na pesa hizo zirekeshwe haraka iwezekanavyo.

“Huu ni wizi kama wizi mwingine, naagiza hapa RPC kesho kutwa nipewe taarifa kuwa watu wote ambao wanahusika na upotevu wa pesa hizi wako rokapu na watatoka pale tu watakapolipa pesa hizi.

“Mtu atatoka ndani baada ya kulipa deni hili, kama kuna sababu nyingine ambazo ziliwafanya washindwe kuwasilisha pesa hizo, hizo zitajulikana baada ya kila mmoja kukamatwa na kutoa maelezo yake, lakini lazima walipe ili tuweze kufunga hii hoja ya CAG,” amesema Kafulila.

Katika hatua nyingine Kafulila amewapongeza viongozi na watumishi wa halmashauri hiyo kwa kupata hati safi, ikiwemo kufikia asilimia 100 ya upelekeaji wa asilimia 10 kwenye makundi maalumu, lakini pia kufikia asilimia 97 ya upelekeaji fedha za maenedeleo asilimia 40.

“Niwapongeze Mkurugenzi wa Halmashauri, watalaamu, madiwani kwa utendaji kazi wenu mkubwa, hakika najivunia kuwa na viongozi kama nyie, mmefanya kazi kubwa na kuna nidhamu kubwa ya matumizi ya fedha za Umma,” amesema Kafulila.

Awali, akisoma taarifa ya CAG Mkaguzi Mkuu wa mkoa, Gwamaka Mwakyosi amesema kuwa Halmashauri ya Busega imepata hati inayoridhisha yenye mambo ya msisitizo, ambapo kulikuwe na hoja 94 huku 52 zikiwa zimefanyiwa kazi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles