23 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Kabudi atuma ujumbe nchi zinazonyanyasa madereva wa malori kwasababu ya corona

 MWANDISHI WETU -DAR ES SALAAM

WAZIRI wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof Palamagamba kabudi, ameziomba Nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kuwapa heshima na kuthamini utu wa madereva wanaosafirisha bidhaa na huduma kuvuka mipaka wakati huu wa mlipuko wa corona.

Profesa Kabudi ametoa wito huo ambapo madreva wa Tanzania na wanchi nyingine, wakilalamika kunyanyaswa na vyombo vya ulinzi vya baadhi ya nchi, kupigwa na kubaguliwa wakidaiwa kusambaza corona.

Alisema hayo jijini Dar es salaam wakati akifungua mkutano wa baraza la mawaziri wa SADC kwa njia ya video katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam.

Alisema nchi wanachama zinapaswa kuchukua hatua za kukabiliana na ueneaji wa virusi vya corona bila kuwanyanyapaa madereva na kuwachukulia kama watu wanaosambaza virusi hivyo. 

“Madereva wetu wamevunjika moyo kwa sababu wanaonekana kama wao ndio wanaosambaza virusi vya corona na si askari wazuri ambao wanatoa huduma ya kusafirisha huduma na biidhaa muhimu wakati huu wa mlipuko, katika nchi za jumuiya,”alisema.

Profesa Kabudi aliziomba nchi za SADC kuwapa heshima na kuthamini utu wa madereva hao huku zikiendelea kuchukua tahadhari za kupambana na janga la corona. 

“Naziomba nchi zetu tuwape heshima na kuthamini utu wa madereva hao na kuwapa heshima wanayostahili huku tukiendelea kuchukua tahadhari zinazotolewa na wataalamu wa afya katika kukabiliana na janga hilo,” alisema.

Prof. Kabudi amesema janga la corona linaonekana kama halitoisha ndani ya muda mfupi na nchi za ukanda wa SADC lazima ziishi kwa kufuata mifumo salama katika biashara na usafirishaji wa huduma na bidhaa ili kupata ukuaji wa uchumi.

Alisema wakati hatua za kukabiliana na janga hilo zikiendelea nchi za SADC lazima zikumbuke dhumuni la utangamano miongoni mwa nchi wanachama ambalo ni kuboresha ufanyaji biashara baina ya nchi na nchi.

Alisema ufanyikaji wa biashara ndani ya SADC uko chini ya asilimia 20 hali ambayo inazuia nchi wanachama kuona ukuaji wa uchumi wake na kuongeza kuwa janga la corona lichukuliwe kama kichocheo cha kuongeza juhudi za kuinua kiwango cha ufanyaji wa biashara baina ya nchi na nchi kupitia utekelezajia wa protokali ya SADC katika biashara ya 2005 na uanzishwaji wa eneo huru la biashara la SADC. 

“Nawaomba nchi zote wanachama wa SADC tuimarishe umoja na mshikamano wetu wakati huu wa kuenea kwa corona, huku bidhaa na huduma muhimu zinazovuka mipaka baina ya nchi na nchi zikiendelea kutolewa, huu ni wakati wa kuepuka vitendo vya kujitenga na kuongeza mashauriano baina ya nchi,”alisema.

Katika mkutano huo, ujumbe wa Tanzania ulioongozwa Prof. Kabudi, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Isack Kamwele, Waziri wa Maliasilia na Utali. Hamisi Kigwangala na Waziri wa Viwanda na Biashara, Innocent Bashungwa.

Nchi zinazoshiriki Mkutano huo ni Angola, Afrika Kusini, Botswana, Malawi, Lesotho Comoro, Eswatini, Mauritius, Msumbiji, Madagascar, Namibia, Visiwa vya Shelisheli, Zambia, Zimbabwe na mwenyejikiti Tanzania.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles