27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

JPM, Museven kuzindua kongamano la biashara Dar

Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Rais John Magufuli Rais amemualika, Rais wa Uganda, Yoweri Museveni kuzindua kongamano la kwanza la biashara kati ya nchi hizo mbili.

Kongamano hilo la biashara kati ya Tanzania na Uganda linatarajiwa kufanyika Septemba 6-7 mwaka huu katika kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Viwanda na Biashara, Innocent Bashungwa amesema Rais Museveni ataambatana na wafanyabiashara kutoka nchini kwake ili kukutana na wafanyabaishara wa Tanzania na kueleza kuwa lengo la kongamano hilo ni kutangaza fursa na kuhamasisha biashara na uwekezaji zilizoko Tanzania na Uganda.

“Serikali itapata fursa ya kuongea na wafanyabiashara hao ili kuangalia changamoto za kufanya biashara katika nchi hizo mbili. Vile vile Serikali zetu zitashirikiana kuzitatua, kuangalia fursa zilizopo, kuongeza biashara katika nchi hizo mbili na kuhamasisha uwekezaji.

“Sisi Tanzania tumekuwa tukiwauzia chakula na vifaa vya viwandani, kwakuwa tunajenga uchumi wa viwanda ni fursa kwa Watanzania kushiriki kwenye kongamano hilo ambalo litakuwa na tija kubwa kwetu kama nchi,” amesema Bashungwa.

“pamoja na mambo mengine, Bashungwa pia amesema Rais Magufuli analeta wakuu wa nchi mbalimbali ikiwemo Uganda ili kuwaonesha fursa tulizonazo pamoja na kujenga mtandao mpana wa biashara.

Aidha, amesema mbali na kongamano hilo, pia kutakuwa na maonesho ya bidhaa za Tanzania ambapo Watanzania watapata fursa ya kuonesha bidhaa za kilimo na za viwandani, taasisi za umma na sekta binafsi zinazosaidia katika mnyororo wa thamani za biashara.

“Ujio huo wa wafanyabiashara utakuwa ni fursa ya kuunganisha wafanyabiashara wa Tanzania na nchi hiyo kukuza wigo wa biashara, kupata masoko mapya pamoja na kutatua changamoto na kujenga mazingira mazuri zaidi ya kufanya biashara,” amesema.

Katika hatua nyingine Bashungwa amewahamasisha wazalishaji wa bidhaa za kilimo, wafanyabaishara na wamiliki wa viwanda kutoka mikoa yote ya nchini kujitokeza kushiriki.

Amesema mwelekeo wa Serikali ya Tanzania ni kujenga uchumi wa viwanda hivyo ni fursa kwa Watanzania kutumia kongamano hili kwa sababu Serikali inazidi kuweka mazingira wezeshi ya kufanya biashara nchini, kujenga viwanda na kufuatilia masoko mbalimbali lengo ni kutaka uuzaji wa bidhaa nchini Uganda uongezeke.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles