25 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

JPM: MAASKOFU HUBIRINI VIWANDA

ELIZABETH HOMBO NA ASHA BANI-DAR ES SALAAM


RAIS Dk. John Magufuli amewataka maaskofu kuhubiri kuhusu ujenzi wa viwanda nchini ili Tanzania isinunue dawa nje ya nchi.

Alitoa kauli hiyo Dar es Salaam jana wakati wa hafla fupi ya kukabidhi magari 181 kwa Bohari Kuu ya Dawa (MSD), ya kusambaza dawa maeneo mbalimbali nchini.

“Lakini hili tumezungumza, tunaimba, sijui nitumie lugha gani, labda niwaombe maaskofu wajaribu kuhubiri hili kwamba tunahitaji kutengeneza viwanda ili Watanzania wapate ajira.

“Labda niwaombe wahubiri na Watanzania wengine wanaojua kuhubiri vizuri, tuwaeleze Watanzania kwamba tunapoteza Sh bilioni 500 kila mwaka kununulia dawa na vifaa mbalimbali kutoka nje wakati tenda hizi zingebaki hapa.

“Kwa bahati nzuri Global Fund wametupa tenda ya nje ya Tanzania kununua dawa pia ya nchi zote za SADC, lakini tunalalamikia mengine, yale ya maana kwa manufaa ya Watanzania hatuyalalamikii.

“Sijui Watanzania tumelogwa! Basi huyo shetani tumkemee kwa majina yote, jina la Muhammad na Yesu, huyo shetani akashindwe ili Watanzania tujue mahali gani tunatakiwa kwenda,” alisema Rais Magufuli.

Katika hafla hiyo, Rais Magufuli alisema sekta ya afya ni nyeti na muhimu na kwamba bila sekta hiyo ni ndoto kufikia maendeleo ya nchi.

“Vifaa plastic (gloves) tunaagiza nje, mabomba ya sindano tunaagiza nje, tungekuwa na viwanda vyetu hizi Sh bilioni 500 zingerudi hapa, tungekuwa na viwanda hizi fedha Sh bilioni 269 zinazopitishwa na Bunge kwa ajili ya kununulia dawa zingebaki hapa na kutengeneza ajira.

“Inauma ukusanye pesa kwa watu masikini, mama lishe, wafanyabiashara ndogondogo halafu hizo pesa mnapeleka kwa wawekezaji nje kununua dawa, mnaenda kutengeneza ajira kwa ajili ya wengine, mimi si mbaguzi, lakini hili linaniuma. Sisi tunakuwa ni chombo la kukusanya fedha kwa ajili ya wengine.

“Nawapongeza wafanyakazi wa MSD kwa sababu wakati naingia madarakani mahali palipokuwa na changamoto kubwa ni MSD, waziri kila siku alikuwa ananiambia. Mmeanza vizuri, mimi ni mgumu kupongeza, kweli mmefanya kazi nzuri sana.

“Niliwaambia mfungue maduka lakini msiwape halmashauri, kama ni wafanyakazi waongezeni lakini si kuwapa tena halmashauri, zitapotea. Mimi ninawafahamu TAMISEMI na ndiyo maana nikasema hata dawa ziende moja kwa moja katika hospitali.

“Mkurugenzi nakupongeza sana, najua ulipigwa madongo nikanyamaza, waache wakupige madongo, wewe ndio mkurugenzi wa MSD,” alisema.

Alisema kupatikana kwa magari hayo kumeifanya MSD kuwa na magari 213 kutoka 32 waliyokuwa nayo awali.

 

Kwa habari zaidi jipatie nakala ya gazeti la MTANZANIA.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles