28.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

JPM azindua ndege mpya, awaonya wenye dhambi ATCL

ndegeNa JONAS MUSHI

-DAR ES SALAAM

RAIS John Magufuli amezindua ndege mbili mpya zilizonunuliwa na Serikali na kutaka watu waliosababisha Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) lishindwe kujiendesha waondolewe mara moja.

Alisema viongozi na wafanyakazi walilihujumu shirika kwa kugawana malipo ya ziada ya usafiri na kutumia mawakala katika kukata tiketi.

Rais aliiagiza Bodi mpya ya ATCL na Mkurugenzi kutotumia mawakala katika shughuli za shirika.

Katika maagizo hayo,   Rais pia amepiga marufuku viongozi wa Serikali kusafiri bure katika  ndege za shirika kama ilivyokuwa awali.

“Viongozi wote lazima walipie nauli hata kama ni mimi. Hata kama ni Waziri atoe nauli kwa sababu hii ni biashara na mwisho wa siku tutawapima kwa kazi,”alisema.

Rais aliyasema hayo alipokuwa akizindua ndege hizo mpya aina ya Bombadier Q400 katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA)   Dar es Salaam jana.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa  taifa akiwamo Spika wa Bunge, Job Ndugai na Katibu Mkuu Kiongozi, John Kijazi.

Rais Magufuli alitumia muda mwingi kueleza sababu ya ATCL kushindwa kujiendesha huku akitaja ubadhirifu na hujuma zilizokuwa zinafanywa na wafanyakazi wa shirika hilo kuwa ndiyo chanzo cha matatizo hayo.

“Naomba nieleze madhambi yaliyokuwa yanafanywa na ATCL iliyokuwapo ikiwa ni pamoja na kushindwa kujitegemea na kujiendesha kwa biashara.

“Badala yake ilitegemea serikali kuiendesha ikiwamo kulipa mishahara” alisema Rais Magufuli na kuongeza:

“Wafanyakazi walibweteka na kufanyakazi kwa mazoea, viongozi na wakurugenzi walijilipa posho za nauli Sh 50,000 kwenda kukagua shughuli za shirika huku likishindwa kukuza uchumi na utalii ambayo ndiyo malengo ya kuanzishwa kwake.

“Bodi na Mkurugezi naomba mjipange vizuri na msitumie mawakala.  Tumieni wafanyakazi wenu lakini mzingatie huduma nzuri”.

Pia  aliwalaumu  viongozi ATCL kuwa waliajiri wafanyakazi pandikizi wa mashirika shindani ambao hawakufanya kazi kwa uaminifu wakiwamo wahandisi na wahasibu.

“Ilipofika katika ukataji wa tiketi watu wanaambiwa ndege imejaa ili waondoke wakapande ndege za kampuni nyingine na ndege yetu inaondoka na abiria watatu.

“Nawaambia bodi hili mlijue maana mnakwenda kufanyakazi na watu wa ajabu,”alisema Rais Magufuli.

Alitaja wizi mwingine uliokuwa unafanywa katika eneo la ukataji wa tiketi kuwa ni watu wazima kusafiri kwa tiketi za watoto, jambo lililolikosesha shirika mapato.

Alitaja vituo vilivyokithiri kwa udanganyifu kuwa ni   Comoro, Mwanza, Dar es Salaam na Mtwara.

Alisema watendaji walisababisha hasara za makusudi huku akitoa mfano wa ndege iliyokaguliwa na kuonekana ina tatizo la tairi lakini ikaruhusiwa kufanya safari.

Ndege hiyo iliharibika ikiwa njiani na abiria wakakodiwa ndege nyingine kwa dola za Marekani 6000, alisema.

Alitaja makosa mengine kuwa ni upotevu wa Sh milioni 700 katika Kituo cha Comoro na muhusika kutochukuliwa hatua badala yake akaongezewa muda wa kufanyakazi baada ya kustaafu.

Makosa mengine aliyataja kuwa ni kutofuata ratiba na kurekodiwa kwa matumizi ya mafuta huku ndege zikiwa hazijafanya safari.

Kutokana na upungufu huo, Rais aliutaka uongozi wa ATCL kuchuja wafanyakazi wake na kuwataka wale wanaotaka kuendelea kufanya kazi kutubu makosa yao na kufanya kazi kwa bidii.

Rais   alibeza watu wanaokejeli aina hizo za ndege kuwa hazina kasi na kuhoji kwa nini serikali imezinunua kwa fedha taslimu.

Akitetea uamuzi huo, alisema ndege hizo zinatofautiana kasi kwa dakika chache na zinatumia mafuta kidogo.

Rais alisema  serikali ilizinunua kwa fedha tasilimu kwa sababu ilikuwa na fedha hizo na kwamba kununua kwa mkopo kungegharimu fedha nyingi zaidi.

“Kwa kutumia ndege za Jet kwenda hadi Songea inagharimu mafuta ya Sh milioni 28.9 lakini hizi (Bombadier Q400) zitatumia mafuta ya Sh milioni moja,” alisema na kuongeza:

“Watu wanaofanya biashara ndiyo wanaopiga vita, ndiyo maana nikasema anayetaka kasi akapande ndege za jeshi.”

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles