27.5 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

JPM AMETUPUNGUZIA KAZI 2020 – UVCCM

Rais Dk. John Magufuli

Na MWANDISHI WETU-KIGOMA

UMOJA wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), umesema kuwa kazi kubwa inayofanywa kwa sasa na Rais Dk. John Magufuli, imeipunguzia kazi CCM katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020.

Kwamba Watanzania wamekuwa wakivutiwa na utendaji kazi wa kiongozi huyo wa nchi ikiwamo kusimamia rasilimali za nchi.

Kauli hiyo imetolewa jana wilayani Uvinza mkoani hapa na Kaimu Katibu Mkuu wa UVCCM, Shaka Hamdu Shaka, alipokuwa akizungumza na wana-CCM kwenye mkutano wa ndani uliofanyika katika kata za Kazuramimba na Nguruka.

Alisema kwa sasa njia imekuwa nyeupe kuelekea mwaka 2020 kwani kazi kubwa inayofanywa na Rais Magufuli ni kielelezo tosha kwa kiongozi huyo kuwa anastahili kupewa nchi na kuongoza kwa awamu ya pili.

Shaka aliwataka wanachama wa CCM kutobweteka na uhakika huo na badala yake wajitume kwa bidii, kufanya kazi ya kisiasa kisayansi na kizalendo kama njia ya kuwatumikia Watanzania wote.

“Utendaji wa Serikali ya Rais Dk. John Magufuli katika kipindi kifupi, kwa hakika umewakosha Watanzania pamoja na kuitikisa dunia na kwa sasa wanyonge nao wanajiona wana thamani na hadhi katika nchi yao.

“Dk. Magufuli ametupunguzia hekaheka na kazi nzito ya kusaka kura za ushindi wa mwaka 2020, hata viongozi na wanachama wa CCM tusibweteke na kujiamini, wajibu wetu ni kufanya kazi na kuwatumikia wananchi,” alisema.

Aidha Shaka alivichambua vyama vya upinzani na kusema vingine ni mabaki ya ukoloni mamboleo katika ardhi ya Tanzania.

Alisema vyama hivyo vimekuwa vikiongozwa na wanasiasa uchwara waliojitahidi kwa miaka mingi kuvipinga vyama vya TANU, ASP na Serikali baada ya Uhuru wa Tanganyika mwaka 1961 na Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964.

Shaka alisema kwa sasa upinzani uliokuwapo nchini hauna lolote zaidi ya kupoteza muda kutokana na vyama hivyo kurithi sera na mipango ileile ya wakoloni na Sultan kwa kuwagawa wananchi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles