Mwandishi wetu-Dar es Salaam
MEYA wa Jiji la Dar es Salaam, Isaya Mwita, amesema changamoto iliyopo katika usafiri wa mabasi yaendayo haraka, itatatuliwa na Jiji hilo na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Tamisemi, Sulemani Jafo, atatoa kibali cha kuendesha mradi huo.
Aliwaomba radhi wananchi ambako wanapata changamoto hiyo na kusema hata jiji halijafurahishwa na adha hiyo na iwapo watapewa kibali kutoka serikali kuu wataimaliza kwa kuwa fedha zipo.
Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kukutana na ugeni kutoka Kisumu, Kenya, Meya Mwita alisema Jiji lina fedha ya kuendesha mradi huo kuondoa adha ya foleni na changamoto wanayokutana nayo wananchi kwa sasa.
Alisema Jiji lina fedha ya kununua mabasi zaidi ya 100 ambayo yanaweza kusaidia kupunguza adha iliyopo kwa sasa na kusisitiza kuwa wanasubiri kibali kutoka Tamisemi waweze kuwa sehemu ya waendesha mradi huo.
“Kwetu sisi kama Jiji tuna fedha za kuendesha huo mradi, hata kama hatutamaliza changamoto, lakini malengo yetu ni kuondoa hiyo adha ya usafiri wanayopata wananchi, niwaombe sana wawe wavumilivu,”alisema.
Alisema adha wanayoipata wananchi inatokana na mabasi kuwa machache na kwamba iwapo mabasi yataongezwa, changamoto hiyo itakuwa imetatuliwa.
“Tunasubiri Tamisemi wao watupe baraka za kuendesha mradi huo kwa kuwa fedha zipo, leo hii hatuwezi kusema kwamba tutafanya bila kupewa kibali.
“Huu mradi ni wa kisasa ndiyo maana wenzetu wamekuja kujifunza kutoka kwetu, niwaombe radhi wananchi wa jijini hapa kutokana na adha hiyo wanayoipata ila baada ya kipidi kifupi haitajitokeza tena,” alisema Meya Mwita.
Katika hatua nyingine, Meya Mwita alisema ugeni huo wa watu 27 umekuja jijini hapa kwa lengo la kujifunza mambo mbalimbali ya maendeleo jijini hapa na kwamba moja ya mambo waliyoyafurahia ni kuhusiana na mradi wa mabasi ya mwendo kasi.