25 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Je inawezekana kuwazuia al-Shabab ?

 Moses Rono

Shambulio lililotekelezwa na wapiganaji wa Kisomali jijini Nairobi Januari 15 mwaka huu ni mapinduzi makubwa ya Propaganda kwa upande wa wapiganaji hao na kuibua wasiwasi kuhusu uwezo wa Kenya kukabiliana na ugaidi.

Wapiganaji hao walitumia vilipuzi na risasi kuingia katika hoteli ya kifahari ya DusitD2 na ofisi nyengine zilizopo katika eneo la Riverside Drive 14 katika eneo la Westlands, karibu na duka la jumla la West Gate Mall ambalo lilishambuliwa 2013.

Mnamo Januari 16, Rais Uhuru Kenyatta alisema kwamba watu 14 waliuawa katika shambulio hilo na kwamba magaidi wote waliangamizwa.

Kanda za kamera za CCTV zilizopeperushwa hewani na vyombo vya habari viliwaonyesha watu wanne waliokuwa wamevalia magwanda meusi wakifyatua risasi za rashasha walipokuwa wakiingia katika hoteli hiyo.

Kundi la Al-Qaeda linalohusiana na wapiganaji wa al-Shabab waliodai kutekeleza shambulio la Westgate Mall ambapo takriban watu 67 walifariki walidai kutekeleza shambulio hilo.

Shambulio hilo lilitokea siku moja baada ya mahakama ya Nairobi kuwashtaki watu watatu kwa mashtaka ya kuwasaidia al-Shabab kutekeleza shambulio la Westgate.

Hoteli ya DusitD2 inarudisha kumbukumbu ya uwezo wa al-Shabab kushambulia ndani ya Kenya, kinyume na madai ya serikali kwamba wanajihad hao wamezuiliwa katika maeneo ya mpakani na Somalia.

Nchini Somalia, kundi la al-Shabab linasalia kuwa tishio kubwa la usalama licha ya operesheni za hivi majuzi za kijeshi na mashambulio ya angani yaliotekelezwa na vikosi vya usalama, wanajeshi wa Muungano wa Afrika AU na vikosi vya Marekani. Kundi hilo la Kijihad linadhibiti maeneo mengi ya Somali ya kati pamoja na kusini.

Kwa nini Kenya inalengwa? Al-Shabab iliimarisha mashambulio yake nchini Kenya wakati serikali ilipotuma wanajeshi wake nchini Somalia kukabiliana na kundi hilo 2011.

Wapiganaji hao waliitaka Kenya kuondoka nchini humo na kuapa kulipiza kisasi. Wito wa serikali kuondoa wanajeshi wake nchini Somalia umekandamizwa na madai kwamba ujumbe huo una wajibu wa kizalendo.

Wengine wamesema kuwa kuondoka kwa wanajeshi wa Kenya nchini Somalia ni sawa na ushindi wa al-shabab.

Mamia ya wanajeshi wa Kenya wameuawa na wapiganaji wa Alshabab nchini Somalia katika kipindi cha miaka minane iliopita.

Serikali imetetea uwepo wa wanajeshi wake nchini Somalia licha ya wito wa mara kwa mara wa kutaka kuondoka kwa mpangilio, ambao baadhi ya wanaharakati wanasema haufanyiki.

Je raia wa Kenya wenye mizizi yao Somalia watashutumiwa? Kufuatia shambulio hilo, vikosi vya ujasusi pamoja na washirika wao wa magharibi watalazimika kukabiliana na seli za kigaidi nchini.

Huenda kukawa na shinikizo ya kuangazia upya kitengo cha ujasusi ili kujilinda dhidi ya mashambulio mengine katika siku za usoni.

Vikosi vya usalama vimepongezwa kwa kuchukua hatua mwafaka ikilinganishwa na hatua walizochukua wakati wa shambulio la West Gate ambalo lilitajwa kuwa janga.

Haitarajiwi kwamba kutakuwa na vita dhidi ya Waislamu ama hata dhidi ya raia wa Kisomali kufuatia shambulio hilo.

Hata hivyo mamlaka itakuwa katika shinikizo la kujadiliana na jamii hizo zaidi ili kusaidia katika ujasusi.

Waislamu na raia wa kabila la Somali katika siku zililzopita wamelalamika kuhusu kukandamizwa na kunyanyaswa na vikosi vya usalama. Wakati huohuo wito wa serikali kuondoa wanajeshi wake Somalia huenda ukaanza tena kutolewa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles